Kapama akwepa wajeda

KIRAKA Nassor Kapama ameachana na ofa ya wajeda (Mashujaa Fc) na kuamua kwenda kujiunga na klabu ya Mtibwa Sugar kwa mkataba wa miezi sita.

Kapama amefikia hatua hiyo baada kuvunja mkataba wake na Simba ambao ulikuwa umesalia miezi sita.

Awali Uongozi wa Simba ulitaka umtoe kwa mkopo lakini kiraka huyo aliomba kuvunjiwa mkataba wake moja kwa moja.

Mwanaspoti linafahamu kiraka huyo kwa sasa bado yupo Dar es Salaam na muda wowote atatimkia mkoani Morogoro kujiunga na timu hiyo.

Kapama alisajiliwa na Simba akitokea klabu ya Kagera Sugar na amehudumu kwenye timu hiyo kwa mwaka mmoja na nusu.