Ishu ya Kyombo ipo hivi kwa Singida

Ishu ya Kyombo ipo hivi kwa Singida

USAJILI wa straika mpya wa Simba, Habibu Haji Kyombo ulikuwa na utata ndani yake baada ya hapo awali kutambulishwa kama mchezaji wa Singida Big Stars zamani DTB.
Kuliibuka maneno mengi ikiwemo kupinga habari iliyoandikwa na Mwanaspoti kuwa Kyombo amesaini mkataba wa miaka miwili na Simba ili kuitumiki msimu huu.
Kyombo alisema sakata la usajili wake alianza kufuatiliwa na Singida ambayo alikubaliana nayo hadi kusaini mkataba wa kuitumikia timu hiyo kwa muda wa miaka miwili.
Alisema baada ya muda likatokea dili lingine kubwa la lenye maslahi mazuri la Simba ilikuwa ngumu kwake kukataa kwa maana hiyo aliwafuata Singida na kueleza hilo ili wakubali kumuachia.
“Nakumbuka tupo kwenye mazingumzo ya kuachana kwa amani na Singida walitoa zile picha za kunitambulisha, halikuwa tatizo kubwa kwa upande wangu ila baada ya kuelewana nao walikubali kuniachia,” alisema Kyombo na kuongeza;
“Nakumbuka wakati huo kila kitu changu kilienda vizuri ikiwemo Simba kuongea vizuri na Singida na kutambulishwa klabuni hapa.
“Kiukweli Tanzania hakuna ambaye hapendi au hana malengo ya kucheza klabu kubwa kama Simba.”