Gomes asambaratisha kikosi chake, Bocco, Mugalu na Ndemla wang'ara

Muktasari:

Katika mazoezi hayo, Gomes aliwapumzisha wachezaji waliocheza jana dhidi ya Mwadui na kuwapa nafasi nyota ambao hawakutumika na waliocheza dakika chache.

Mwanza. Kikosi cha Simba kimefanya mazoezi yake kujiandaa na mchezo wao dhidi ya Kagera Sugar, huku ikishuhudiwa nyota waliocheza mechi ya jana kwa dakika 90 wakikosekana.

Matizi hayo ambayo yamefanyika leo Jumatatu katika uwanja wa Nyamagana jijini hapa, yalihusisha wachezaji ambao hawapati namba na ambao jana dhidi ya Mwadui walicheza dakika 45 na wengine kutokea benchi.

Wachezaji kama Kipa Aish Manula, Shomari Kapombe, Mohamed Hussein, Joash Onyango, Paschal Wawa, Erasto Nyoni, Clautous Chama, Rally Bwalya na Medie Kagere hawakuonekana kabisa katika mazoezi hayo.

Mazoezi hayo ambayo yalitumia takribani masaa mawili huku kimvua pia kikiambatana humohumo, ilishuhudiwa wachezaji ambao hawajapata namba kwa muda mrefu na wengine waliocheza dakika 45 au pungufu wakipiga jalamba la maana.

Nyota walioonekana ni pamoja na John Bocco ambaye pia aliweza kufunga bao safi, Chris Mugalu alitetupia mawili, Beno Kakolanya, Ally Salim, Ibrahim Ajibu, Jonas Mkude na Ibrahim Amme.

Wengine ni Duchu Kameta, Francis Kahata, Kennedy Juma, Benard Morison, Miraji Athuman, Hassan Dilunga, Luis Miquisone na Said Ndemla aliyetupia bao.

Akizungumza baada ya mazoezi hayo, kocha wa timu hiyo Didier Gomes amesema wachezaji wote kwa sasa wana umuhimu na kwamba kutoonekana kwa baadhi mazoezini ni kutaka kuona uwezo wa wale ambao hawakucheza jana.

Amesema amefurahishwa na uwezo wa nyota wake na kwamba wanaenda kupambana kuhakikisha mchezo dhidi ya Kagera Sugar wanashinda ili kuendelea kujiweka nafasi nzuri na kwamba malengo yao ni kuvuna alama tisa kanda ya ziwa.

"Kila mchezaji ana umuhimu wake kwa kila mchezo na hawa ambao hawapo walikuwa na mechi jana kwahiyo lazima tuangalie kila mmoja kwa faida ya timu, tunajua Kagera Sugar ni timu nzuri hivyo tunaenda kupambana" amesema Gomes.