Fei asaka rekodi za Bocco, Kipre Tcheche

Muktasari:

"Sitaki kushindanishwa na mtu, nawaheshimu wenzangu waliotangulia na wamefanya kazi nzuri kwa upande wao, mimi pia natakiwa kuandika rekodi yangu, ili watakaokuja nyuma yangu wawe na kitu cha kunisimulia ndivyo ulivyo mchezo wa soka," alisema.

BAADA ya kiungo wa Azam FC, Feisal Salum 'Fei Toto' kuyafikia mabao 14 aliyofunga, Prince Dube msimu wa 2020/21, amebakiwa na mitihani miwili ndani ya kikosi hicho.

Fei Toto ambaye huu ni msimu wake wa kwanza kucheza Azam, ndiye kinara wa mabao (14) kwa chama hilo, pia ametoa asisti sita, ingawa anayeongoza kwa asisti ni Kipre Junior aliye nazo nane.

Ndani ya kikosi cha Azam kulikuwa na mastaa wawili ambao walishaondoka kwa nyakati tofauti, wakiwa wameacha rekodi zao za mabao ambazo bado hazijavunjwa.

Mshambuliaji John Bocco msimu wa 2011/12 alifunga mabao 19 na msimu uliofuata (2012/13) Kipre Tcheche alimaliza kinara wa ligi kwa mabao 17.

Bocco kwa sasa anaichezea Simba na Kipre yupo Kuching City, endapo Fei Toto akiendelea na kasi ya ufungaji huenda akavunja rekodi za malegendari waliomtangulia.

Ukiachana na Fei kukabiliana na mtihani wa Bocco na Kipre, pia ni muda mrefu Azam FC haijatoa kinara wa mabao katika Ligi Kuu tangu walivyofanya Bocco na Kipre.

Fei Toto alizungumzia hilo, alisema kwa upande wake anaona hawezi kushindana na mchezaji yeyote awe amemtangulia ama anacheza naye.

"Sitaki kushindanishwa na mtu, nawaheshimu wenzangu waliotangulia na wamefanya kazi nzuri kwa upande wao, mimi pia natakiwa kuandika rekodi yangu, ili watakaokuja nyuma yangu wawe na kitu cha kunisimulia ndivyo ulivyo mchezo wa soka," alisema.