Dk Devotha amrithi Kibira Chaneta

Muktasari:

  • Kibira alienguliwa kwenye usaili uliofanyika juzi Ijumaa, lakini Katibu Mkuu wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Mohamed Kiganja alisema atabaki kuwa mshauri wa Chaneta.

Dk Devotha Marwa ameteuliwa kwa mwenyekiti mpya wa Chama cha Netiboli Tanzania akichukua nafasi ya Anna Kibira aliyeenguliwa kwenye usaili.

Kibira alienguliwa kwenye usaili uliofanyika juzi Ijumaa, lakini Katibu Mkuu wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Mohamed Kiganja alisema atabaki kuwa mshauri wa Chaneta.

Katika uchaguzi uliofanyika jana Jumamosi, Dk Devotha ndiye alipewa ridhaa na wapigakura ya kuiongoza Chaneta kwa miaka minne akimshinda Damian Chonya.

Anna Gidelya aliteuliwa kuwa makamu mwenyekiti akichukua nafasi ya Zainabu Mbiro ambaye kwenye uchaguzi wa sasa aliwania nafasi ya katibu mkuu lakini akaangushwa na Judith Irunda huku Hilda Mwakatobe akiteuliwa kuwa Katibu msaidizi.

Upande wa wajumbe, Mohamed Kilongozi, Luiza Jela, Yasinta Silvester, Fortunata Kabeja, Julieth Mdeme na Asha Sapi waliibuka kidedea na Grace Khatibu aliyekuwa anagombea nafasi ya mweka hazina akikosa baada ya kupigiwa kura nyingi za hapana.

"Chaneta watafanya uchaguzi mdogo kuziba nafasi hiyo baadae," alisema Kiganja akifafanua nafasi ya mweka hazina itakavyozibwa.

Awali, BMT ilitoa sababu za kumuengue kwamba, "Tumemuengua Kibira kwa kuwa tumeona hataweza mikiki mikiki ya netiboli kutokana na afya yake," alisema Kiganja.

Naye Kibira alizungumza sakata hilo akisema, "Yote nimeamua kumwachia  Mungu, najua ilipangwa iwe hivyo, nitaendelea kutoa mchango wangu Chaneta pale itakapohitajika."