Diego bado kidogo Yanga

Soffou Boubacar ‘Diego’.

Muktasari:

Pluijm aliyemwingiza Boubacar katika pambano lao la juzi Jumamosi dhidi ya Mbeya City, lakini kabla ya mchezo huo kwenye mazoezi ya timu hiyo alionekana kumweka Diego katika kikosi cha pili sambamba na straika mpya Paul Nonga.

KOCHA Mkuu wa Yanga, Hans Pluijm, ameonyesha ukomavu kwa kugoma kuharakisha mambo katika kumwingiza katika kikosi cha kwanza kiungo wake mpya, Soffou Boubacar ‘Diego’, ila akafichua mambo matatu matamu alionayo Mniger huyo.

Pluijm aliyemwingiza Boubacar katika pambano lao la juzi Jumamosi dhidi ya Mbeya City, lakini kabla ya mchezo huo kwenye mazoezi ya timu hiyo alionekana kumweka Diego katika kikosi cha pili sambamba na straika mpya Paul Nonga.

Kikosi kingine cha kwanza safu ya ushambuliaji iliongozwa na washambuliaji Donald Ngoma na Amissi Tambwe na viungo wa pembeni wakiwa Simon Msuva na Deus Kaseke ambaye alionekana katika winga ya kushoto nafasi inayotumiwa na Diego.

Akizungumza mara baada ya mazoezi hayo, Pluijm aliliambia Mwanaspoti kuwa tayari kuna mambo matamu ameanza kuyaona kwa Diego yakiwemo krosi zake tamu na ujuzi wa kumiliki na kuchezea mpira.

Pluijm alisema mbali na mambo hayo Diego pia ameonyesha anajua kupenya na mipira ambapo sasa bado jambo moja ambalo ni kumudu kasi ya soka la kikosi hicho jambo ambalo atalizoea taratibu.

“Tayari ameonyesha kuna vitu ambavyo vitatusaidia angalia anavyojua kumiliki mpira lakini pia anajua kufanya vitu flani adimu na usisahau ujuzi wake wa kutengeneza krosi safi ni kati ya vitu ambavyo anavyo na tulikuwa tunavitaji,” alisema.

“Najua watu wangependa kumuona haraka, ila tayari tuna kikosi kipana ambacho tunaweza kukitumia kushinda.”