Chama aifuata Mbeya City

KIKOSI cha wachezaji 26 akiwemo kiungo Clatous Chama kinatarajiwa kuondoka Dar es Salaam leo mchana kuelekea Mbeya tayari kuwakabili Mbeya City katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Simba ni mgeni wa Mbeya City mchezo utakaopigwa uwanja wa Sokoine Jumatatu ikiwa ni mchezo wao wa 11 baada ya ule dhidi ya Kagera Sugar kufutwa kutokana na wachezaji wao kuwa wagonjwa.
Baada ya Simba kurejea jana kutoka Zanzibar katika michuano ya Mapinduzi wachezaji wao walipewa mapumziko mafupi kwa ajili ya kuonana na familia zao na leo wamerejea asubuh kuendelea na majukumu.
Kwa mujibu wa taarifa ya Simba, mchezo huo wameupa kipaumbele kikubwa kwa kuwa wanahitaji pointi tatu katika kila mchezo ambao watakutana nao.
Aidha baada ya kuwasili Mbeya leo, kikosi kitafanya mazoezi ya utimamu wa mwili na kesho mazoezi ya mwisho kabla ya mchezo huo.