Baraza asaini miaka miwili na nusu Kagera Sugar

Muktasari:

  • Kocha huyo alitua nchini msimu uliopita na sasa amejiunga na Kagera Sugar ikiwa ni timu ya pili kwake katika Ligi Kuu.

Mwanza. Kocha FrancisĀ  Baraza amethibitisha kutua Kagera Sugar kwa mkataba wa miaka miwili na nusu na wiki ijayo ataanza kuitumikia timu hiyo ya mjini Bukoba.

Kocha huyo raia wa Kenya amejiunga na timu hiyo akichukua mikoba ya mtangulizi wake, Mecky Maxime ambaye alivunjiwa mkataba na benchi lake na mabosi wake kwa madai ya kutofurahishwa na matokeo kwenye Ligi Kuu .

Hata hivyo Kocha huyo licha ya kuondoka ndani ya Biashara United, ameiachia mafanikio ikiwa ni kuwa nafasi ya nne kwa pointi 39 kwenye msimamo wa ligi na kuiwezesha kufuzu hatua ya 16 bora ya michuano ya kombe la shirikisho.
Baraza ameliambia Mwanaspoti kuwa tayari ameaga katika klabu yake ya zamani, Biashara United na sasa atakuwa katika majukumu mapya kuendeleza kazi yake.

"Nimeaga tayari Biashara United, ngoja nipate changamoto mpya, hata nilikotoka nilipakuta pakiwa kama ninakoenda, hii ni kazi yangu wala siogopi chochote" amesema Baraza.