Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Balaa la Yanga... Yaibua hoja nne, kinachofuata hiki hapa

Muktasari:

  • Katika kikao hicho kilichofanyika jijini Dar es Salaam na kutumia dakika 143, Yanga waliibua hoja mpya nne kukandamizia msimamo wao wa awali wa ‘hatuchezi’ na wakaenda mbali zaidi kwamba wasiposikilizwa hawaingizi timu uwanjani kuanzia sasa.

KWA tafsiri nyepesi ni kwamba ngoma bado ni ngumu. Hatma ya Dabi ya Kariakoo bado ipo rehani haswa kutokana na misimamo na hoja za Yanga walizotoa baada ya kikao cha jana Jumatatu walipokutana na Bodi ya Ligi (TPLB).

Katika kikao hicho kilichofanyika jijini Dar es Salaam na kutumia dakika 143, Yanga waliibua hoja mpya nne kukandamizia msimamo wao wa awali wa ‘hatuchezi’ na wakaenda mbali zaidi kwamba wasiposikilizwa hawaingizi timu uwanjani kuanzia sasa.

Huku Yanga wakisisitiza dabi haipo, Mwanaspoti linajua kwamba Simba wamepigiwa simu na kutakiwa kuripoti kambini kuanzia jana Jumatatu jioni kwa maandalizi ya mchezo huo ulioahirishwa Machi 8 na Bodi ya Ligi saa chache baada ya Simba kutishia kutoicheza kutokana na kuzuiwa kufanya mazoezi ya mwisho kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa na wanaodaiwa kuwa makomandoo wa Yanga.

Simba wamesisitiza kuwa, wanatambua mchezo huo upo na watajiandaa kama wanavyofanya kwenye michezo mingine ya Ligi Kuu Bara, tofauti na Yanga walikaririwa mapema hawataicheza mechi hiyo.

Msisitizo wa Yanga unamaanisha kwamba hata katika mechi za Ligi zilizosalia na fainali ya Shirikisho hawatacheza. Kikao hicho kilianza saa 4:30 asubuhi hadi saa 6:53 mchana, Yanga imeendelea na msimamo mkali wa kugomea mchezo huo wa dabi dhidi ya Simba ikieleza mbele ya uongozi mzima wa Bodi chini ya Mwenyekiti, Steven Mnguto, Makamu Nassoro Idrissa ‘Father’ na Ofisa Mtendaji Mkuu, Almasi Kasongo. Hoja nne za Yanga:


KAMATI YA USIMAMIZI IVUNJWE

Hii ni moja ya hoja zao nzito. Yanga inataka Kamati ya Usimamizi wa Ligi ivunjwe kwa kile ilichodai imeshindwa kusimamia kwa weledi usimamizi wa Ligi kwa msimu wa 2024/25.


KATIBU TFF ANG’OKE

Pili, Yanga pia katika barua yao ambayo Mwanaspoti limeiona, imetaka Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wilfred Kidao kujiuzulu.

Madai yao ni kwamba Mtendaji huyo ameshindwa kuchukua hatua juu ya makosa ya waamuzi wanaochezesha mechi za Ligi kwa kushindwa kutoa haki na wakidai wanaipendelea klabu ya Simba.


OFISA MTENDAJI WA BODI AJIUZULU

Katika msimamo huo, hoja yao ya tatu, Yanga imetaka pia Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi, Almasi Kasongo kuachia ngazi wakidai alipotosha wakati wa kuahirishwa kwa mchezo namba 184 uliopangwa kufanyika Machi 8, 2025.


BODI KUWA HURU

Shinikizo la nne la klabu hiyo ni kutaka kuona Bodi ya Ligi (TPLB) inasimama kama chombo huru kitakachotoa haki kwa taasisi zote na isiingiliwe na mamlaka yoyote kwenye maamuzi.


‘HATUCHEZI LIGI’

Mbali na mambo hayo manne Yanga ukiondoa kutocheza mchezo huo dhidi ya Simba, pia imesema endapo mambo hayo hayatafanyiwa kazi, basi haitacheza mechi zilizosalia za Ligi sambamba na Fainali ya Kombe la Shirikisho (FA) dhidi ya Singida Black Stars mjini Zanzibar.


KASONGO AFAFANUA

Akizungumza baada ya mkutano huo wa Jumatatu, Kasongo amekiri kukutana na Yanga pamoja na kupokea mambo hayo manne ambapo watakwenda kuyafanyia kazi.

Lakini amesisitiza kwamba bado mchezo huo namba 184 uliopangwa kupigwa Juni 15, yaani Jumapili ijayo upo pale pale kama ambavyo ulitangazwa hadi itakapotangazwa tofauti.

“Tumekutana na Yanga kilikuwa ni kikao kizuri chenye kujenga, kama mnavyofahamu Bodi ni chombo cha klabu na tunapokutana ni jambo lenye afya, tumeyapokea mambo manne ambayo wameyaleta na sisi kama Bodi hatua ya kwanza tumeyapokea na baada ya kuyapokea tutakwenda kuyachakata,” alisema Kasongo na kuongeza:

“Katika haya mambo manne ni jambo moja ambalo lipo kwenye mamlaka ya Mwenyekiti wa Bodi ambalo ni muundo wa Kamati ya Usimamizi wa Ligi, lakini haya mengine yanahitaji muda na kuamuliwa kwenye vyombo vingine tofauti.

“Haya yanahitaji muda kuweza kupata muafaka wake hayawezi kufanyika kwa haraka hata kama ukitaka kuyafanyia kazi kwa hiyo kwa mamlaka yangu au wa nafasi yangu naweza kusema ratiba inabaki vilevile kama ambavyo ilipangwa mpaka hapo itakapoamuliwa vingine.”


YANGA KIKAONI

Makamu wa Rais wa Yanga, Arafat Haji, Mtendaji Mkuu Andre Mtine na Wajumbe wa Kamati ya Utendaji, Alexander Ngai  na Rodgers Gumbo ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano, Ofisa Habari, Ally Kamwe na Wanasheria watatu wa klabu hiyo ndio walioiwakilisha klabu katika mkutano huo ambao Simba hawakuwa waalikwa.

Mara baada ya mkutano huo, Arafat alisema: “Tulichofanya ni kuwasilisha msimamo wa klabu kutoka kwa wanachama na mashabiki wetu hilo ndio kubwa.”

Awali kabla ya taarifa hiyo, Yanga kupitia katika kurasa zao za kijamii ilisema kuwa viongozi wake walikaa kikao cha saa kadhaa na viongozi wa bodi na kuwasilisha msimamo wa klabu kutoshiriki mechi ya Juni 15, 2025 hadi matakwa yao waliyowasilisha Bodi ya Ligi kwa maandishi yatakapotekelezwa.

Mechi hii awali ilipangwa kupigwa Machi 8, 2025, lakini kabla Simba iliandika barua ya kulalamika kuwa imezuiwa kufanya mazoezi ya mwisho kwenye Uwanja wa Mkapa sehemu ambayo ndio mchezo huo ulikuwa unafanyika na wale wanaodaiwa kuwa makomandoo wa Yanga.

Saa chache kabla ya mechi hiyo, Bodi ya Ligi ilitoa taarifa ya kuahirisha, tofauti na kile alichonukuliwa Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Steven Mnguto mapema asubuhi kwamba mechi hiyo ilikuwa ipo palepale.

Jambo hilo , jambo ambalo liliwaudhi Yanga na kutangaza kuwa hawatacheza mchezo mwingine hadi watakapopewa taarifa rasmi kwanini mechi ya kwanza haikufanyika.


MAHAKAMANI ILITUPWA

Ikumbukwe kuwa, wiki iliyopita Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam ilijiweka pembeni katika kesi ya kuzuia mechi hiyo ya watani wa jadi, Yanga dhidi ya Simba maarufu kama Dabi ya Kariakoo iliyopangwa kuchezwa Juni 15, 2025, baada ya kuamua kuwa haina mamlaka ya kuisikiliza.

Kesi hiyo ilifunguliwa na mwanachama wa Yanga kutoka Iringa, Dk Samweli Marwa Chacha dhidi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu (TFF) na Bodi ya Ligi (TPLB) pamoja akiomba kufutwa kwa ratiba mpya ya mechi hiyo na Yanga ipewe alama tatu.

Hata hivyo, TFF na TPLB kupitia wakili Rahim Shaban iliweka pingamizi la awali dhidi ya kesi hiyo ikidai kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kuisikiliza kesi hiyo.

Mahakama Kuu katika uamuzi wake uliotolewa Ijumaa na Jaji Elizabeth Mkwizu aliyesikiliza pingamizi hilo imekubaliana na hoja za pingamizi la TFF na Bodi na kutupilia mbali kesi hiyo.

Jaji Mkwizu alisema kuwa Katiba ya TFF na ya Yanga ambayo mdai ni mwanachama inazuia wanachama kupeleka masuala ya migogoro ya uendeshaji wa mchezo huo katika mahakama za kisheria, bali masuala hayo yanaweza kushughulikiwa na vyombo vya ndani ya TFF au Mahakama ya Usuluhishi wa Michezo (CAS).


MSIMAMO WA WAZEE

Wanachama wa matawi wakiongozwa na wazee wa klabu hiyo walitoa msimamo mzito wiki iliyopita wakiupiga mkwara uongozi. Wanachama hao walisisitiza kwa kusema; ‘HATUCHEZI’ huku wakitoa hoja mpya kwa mabosi wa klabu hiyo kama wanatakiuka msimamo huo, basi wajue mlango wa kutoka utakuwa wazi.


KITAKACHOIKUTA

Kama Yanga itasimamia msimamo huo wa kutoicheza mechi hiyo ambayo ni ya marudiano ya Ligi Kuu Bara kwa msimu huu baada ya awali kukutana Oktoba 19 mwaka jana na Simba kulala 1-0 kwa bao la kujifunga la beki Kelvin Kijili, klabu hiyo na viongozi wake watakumbana na adhabu kadhaa.

Kwa mujibu wa Kanuni ya Ligi Kuu Namba 47: Udhibiti wa Klabu kifungu cha 18 kinaweka bayana adhabu inayoweza kuikumbua Yanga kwa kukaidi agizo la wenye mamlaka inayosema hivi; “Klabu ambayo itashindwa au kukaidi kutii maagizo/maamuzi au utekelezaji wa maamuzi ya TFF/TPLB itatozwa faini ya shilingi milioni tano (5,000,000/-) au/na kuondolewa kwenye Ligi Kuu na kushushwa daraja.”

Pia Kanuni namba 46: Udhibiti kwa Viongozi kifungu cha 9 kinaweka wazi kwamba; ‘Kiongozi atakayebainika kushindwa/kukaidi kutii maamuzi au maagizo ya TFF/TPLB atafungiwa kwa kipindi kati ya miezi mitatu (3) na miaka mitatu  (3) na kutozwa faini isiyopungua shilingi milioni moja (1,000,000/-)

Wakati kifungu cha 14, kinasema kuwa; ‘Kiongozi atakayebainika kusababisha timu kutofika uwanjani na kukosa mchezo, baada ya kuhudhuria kikao cha maandalizi, atatozwa faini ya shilingi milioni moja (1,000,000/-) na kufungiwa kipindi kisichopungua miezi kumi na miwili (12).

Mbali na kanuni hizo, lakini Kanuni Namba 31: Kutofika Uwanjani imeainisha katika kifungu namba moja kilichosema; Timu yoyote itakayokosa kufika uwanjani bila ya sababu za msingi zinazokubalika kwa TFF/TPLB na/au kusababisha mchezo usifanyike itakabiliwa na adhabu zifuatazo:

1.1 Kutozwa faini ya shilingi milioni tano (5,000,000/-) ambapo shilingi milioni mbili na laki tano (2,500,000/-) itachukuliwa na Bodi ya Ligi Kuu na shilingi milioni mbili laki tano (2,500,000/-) italipwa kwa timu pinzani.

1.2 Kulipa fidia ya maandalizi/uharibifu wowote unaoweza kujitokeza.

1.3 Kupokwa alama 15 (kumi na tano) katika msimamo wa Ligi na viongozi waliosababisha jambo hilo watachukuliwa hatua zaidi za kinidhamu.


MTAZAMO WA TINO, KIEMBA

Kutoka na msimamo huo mpya wa Yanga juu ya Dabi, nyota wa zamani aliyewahi kuzitumikia timu hizo kwa vipindi tofauti, Amri Kiemba alisema; “Kwa Yanga baada ya mechi kuhairishwa walisema mechi wameimaliza kwa muda wote ambao nilikuwa naona sakata hili nilidhani kuwa bodi walikaa chini na Yanga na kumaliza yale malalamiko na kufanyia kazi yale ambayo Yanga ilikuwa inahitaji.

“Kuamua kutumia tu nguvu mechi inachezwa si sawa nadhani nguvu hii ingetumika Machi 8 pengine leo tusingekuwa hapa, walitakiwa kusema mechi itakuwepo wakati huo na ambaye hatakuja sisi tutaendelea na taratibu zetu, akiangalia vitu ambavyo Yanga inahoji bado majibu hayajapatikana.”

Kiemba aliongeza kwa kusema: “Bodi ya Ligi ilisema tu mechi imehairishwa na sababu hali ya usalama na mazingira ya rushwa, Simba ilisema vitu vingine na mechi ilihairishwa na vitu vingine... kwa hiyo wao wanachokiona ni kwamba hawakutendewa haki. Na kama mechi haikuchezwa nani amewajibika, hivyo Yanga inasimamia hilo na kama itafanikiwa kuna ujumbe mzuri ambao watakuwa wametoa.”

Kwa upande wa nyota wa zamani wa kimataifa aliyewahi kuwika na Majimaji Songea, Pan Africans, Yanga na Taifa Stars, Peter Tino alivishauri vyombo vyenye mamlaka ya kuusimamia soka nchini, TPLB na TFF visizichukulia klabu kongwe kama watoto wadogo badala yake maamuzi yanayotolewa kwa timu nyingine iwe hivyo na kwao.

“Mechi ya Simba na Yanga ni kawaida tu kama ilivyo nyingine ila zinavyochukuliwa na TPLB na TFF ndiyo matokeo yake hayo, sikutarajia kama ishu hiyo ingefika hapo, binafsi naona kitendo cha Yanga kugomea mechi kinakwenda kuongeza uimara wa kusimamia kanuni za ligi kikamilifu ,” alisema Tino na kuongeza;

“Nilichogundua kilichosababisha kuahirishwa kwa dabi ya Machi 8 ilikuwa ni kukosekana kwa mawasiliano sahihi ya TFF na TPLB, ila kwa hicho kilichotokea kiwasaidia kufanya maamuzi kwa Simba na Yanga zikiteleza zichukuliwe hatua kama inavyoelekezwa katika kanuni za kusimamia mechi.”