Azam yashusha Mzimbabwe

AZAM imeamka sasa na wao wameanza kubadilisha ndege wakifuata mastaa wao wapya na mtu wa kwanza wakamtanguliza kiungo mmoja Mzimbabwe na yupo pale Chamazi tayari na imemfuata mwingine Zambia.

Azam imemleta kiungo rasta Last Jesi wakitaka kocha wao, George Lwandamina amfanyie tathmini kama anawafaa ili asajiliwe na kwa mashabiki wa soka wanamkumbuka jamaa aliupiga mwingine katia michuano ya Simba Super Cup 2020, alipokuja na Al Hilal ya Sudan.

Kiungo huyo rasta anatarajiwa kuanza majaribio ndani ya Azam mara baada ya kikosi hicho kurejea kutoka Lindi na jana waliifuata Namungo katika mchezo wa Ligi Kuu utakapigwa kesho pale Uwanja wa Majaliwa.

Lakini wakati rasta huyo akitua, Mwanaspoti linafahamu Mtendaji Mkuu wa Azam, Abdulkarim Amin ‘Popat’ yupo Zambia akiwafuata viungo wengine wawili.

Popat amekwenda kumaliza dili la Benson Sakala wa Power Dynamos ambaye yupo katika mawindo yao akiwa pia anaitumikia timu ya taifa ya Zambia.

Katika ripoti ya Lwandamina inahitaji viungo wawili mkabaji na hesabu zipo kwa Sakala, pia Popat akimaliza hapo atahamia kwa mido mwingine wa juu anayejua kuchezesha timu Collins Shikombe.

Shikombe amekuwa katika mawindo ya muda mrefu kwa Azam tangu afanye vuzuri katika Fainali za Mataifa Afrika kwa wachezaji wa ndani na sasa Popat ametua nchini humo kuangalia uwezekano wa kumalizana naye.