Ayoub atwishwa zigo la lawama Kariakoo Dabi

Muktasari:

  • Kwa Aprili tangu 1965, timu hizo zimekutana mara 13 ambapo Simba imeshinda mara nne, huku Yanga ikishinda mara tatu wakati mechi sita zilizobaki zikimalizika kwa miamba hiyo kushindwa kutambiana.

KOCHA wa Simba, Abdelhak Benchikha amemuanzisha kipa  Ayoub Lakred katika mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya watani zao, Yanga.

Ayoub aliyesajiliwa na timu hiyo msimu huu, huo utakuwa mchezo wake wa kwanza wa Dabi ya Kariakoo kucheza tangu aliposajiliwa akitokea klabu ya Far Rabat ya Morocco.

Katika kikosi cha Simba kinachoanza leo dhidi ya Yanga ni Ayoub Lakred, Israel Mwenda, Mohamed Hussein 'Tshabala', Henock Inonga, Che Malone, Babacar Sarr, Fabrice Ngoma, Sadio Kanoute, Clatous Chama, Saidi Ntibanzokiza 'Saido' na Kibu Denis.

Wachezaji wa akiba katika mchezo huu ni Ally Salim, David Kameta 'Duchu', Kennedy Juma, Hussein Kazi, Mzamiru Yassin, Luis Miquissone, Ladaki Chasambi, Pa Omar Jobe na Freddy Michael Koublan.

Simba inakutana na Yanga huku ikiwa na rekodi nzuri ya kushinda michezo mingi wakati zilipokutana kwa mwezi Aprili tangu mwaka 1965.

Kwa Aprili tangu 1965, timu hizo zimekutana mara 13 ambapo Simba imeshinda mara nne, huku Yanga ikishinda mara tatu wakati mechi sita zilizobaki zikimalizika kwa miamba hiyo kushindwa kutambiana.

Katika michezo 13 iliyochezwa kwa Aprili, yamefungwa mabao 29 ambapo Yanga imefunga 15 huku Simba ikifunga 14.