Arsenal yampandisha mzuka Yohana Mkomola

Muktasari:

kwa upande wa mazoezi mengine ya kujiandaa na msimu mpya hayana tofauti na ambayo alikuwa akiyafanya akiwa na klabu yake ya Yanga.

STRAIKA wa zamani wa Yanga, Yohana Mkomola anayekipiga katika Klabu ya Arsenal Kyiv inayoshiriki Ligi kuu ya Ukraine, amefurahishwa kuwa sehemu ya wachezaji wanaojiandaa na msimu mpya.
Mkomola alikuwa katika kikosi cha Yanga, lakini baadaye alipata nafasi ya kwenda kufanya majaribio katika Klabu ya Arsenal Kyiv na alipofuzu majaribio na kusajiliwa.
Mkomola alisema anashukuru kuwa sehemu ya maandalizi kwa ajili ya msimu ujao, kwani anaamini atazidi kuwa fiti kwa kuanza pamoja na wenzake.
“Tupo kwenye maandalizi ya msimu ujao na kila siku tunafanya mazoezi kwa kufuata programu zilizopo, tunachezea sana mipira kila zoezi ambalo tunafanya lazima tuwe na mpira pembeni,” alisema.
Aliongeza kwa upande wa mazoezi mengine ya kujiandaa na msimu mpya hayana tofauti na ambayo alikuwa akiyafanya akiwa na klabu yake ya Yanga.
“Mazoezi mengine ambayo tunafanya ni ya kawaida tu kwa sababu mpira hauna tofauti duniani na sehemu yoyote ile ambayo utaenda kwahiyo hakuna tofauti kubwa sana,” alisema.