Anayesakwa na Arteta afunguka kila kitu

PARIS, UFARANSA. KIUNGO wa Lyon, Houssem Aouar amefichua amegoma kwenda Arsenal kwa sababu anataka kubaki kwenye timu iliyomwibua na kumkuza.

Kocha wa Arsenal, Mikel Arteta alihitaji sana huduma ya kiungo huyo Mfaransa kwenye dirisha la majira ya kiangazi ambalo lilifungwa jana Jumatatu.

Lakini, mazungumzo ya dili hilo yalikatizwa baada ya Arsenal kushindwa kulipa kiwango cha pesa ambacho Lyon ilihitaji kulipwa kwenye mauzo ya mchezaji huyo.

Jana Jumatatu, mashabiki wa Arsenal walikuwa wakisikilizia kama kutakuwa na ofa yoyote ya dakika za mwisho itakuwa imetua huko Lyon kwa ajili ya huduma ya kiungo huyo.

Staa huyo wa Lyon, alipoulizwa kuhusu kushindwa kwenda Arsenal, alisema: “Kwanza kwa sababu nahisi kwamba nahitaji kuendelea kufanya mambo kwenye hii klabu, ni hivyo tu.

“Nataka kuendelea kufanya mambo yangu hapa kwenye klabu hii iliyonikuta. Tunafahamu tunatembelea vichwa juu kwa sababu tunafanya vizuri.”

Aouar aliibukia kwenye timu ya watoto ya Lyon na klabu yake inahitaji Pauni 45 milioni kwenye mauzo yake, huku mchezaji mwenyewe akiripotiwa hakutaka kuondoka kwenye dakika za mwisho kwa sababu ya hofu ya kushindwa kutulia kwenye timu mpya na kupoteza nafasi ya kuwamo kwenye kikosi cha Ufaransa kwenye Euro 2021.

Arteta alikuwa kwenye mchakato wa kutafuta pesa kwa ajili ya kunasa huduma ya mchezaji huyo kabla ya dirisha la usajili kufungwa jana Jumatatu.