Ali Kamwe afunguka ishu nzima ya Pacome, iko hivi

NYOTA wa Yanga, Pacome Zouzoua ameanza rasmi mazoezi na timu hiyo baada ya kukosekana kutokana na majeraha ya goti aliyoyapata wakati wa mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Azam FC.

Katika mchezo huo uliopigwa Machi 17, mwaka huu na kushuhudia Yanga ikifungwa mabao 2-1 kwenye Uwanja Benjamin Mkapa, Pacome alishindwa kuendelea dakika ya 28 tu na alibebwa na kurudishwa nyumbani.

Akizungumza na Mwanaspoti, ofisa habari na mawasiliano wa timu hiyo, Ally Kamwe amesema nyota huyo ameanza mazoezi na anatarajiwa kurudi uwanjani muda wowote kuanzia sasa.

"Hata mechi ya leo na Coastal Union angeweza kucheza lakini benchi la ufundi liliamua kutomtumia ili kumpa nafasi ya kurudi akiwa imara zaidi huko mbeleni," amesema.

Kamwe aliongeza, mchezo ujao wa timu hiyo wa robo fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) dhidi ya Tabora United utakaopigwa Mei Mosi, kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, nyota huyo atakuwa fiti kucheza.