Al Ahly wafunga hesabu kwa Miquissone, Simba kumuaga kesho

Muktasari:

  • Miquissone alijiunga na Simba, Januari 2020 akitokea UD Songo

Uongozi wa Ahly umekamilisha rasmi uhamisho wa winga Luis Miquissone kutoka Simba kwa ada ya Dola 900,000

Usajili wa winga huyo umekamilika rasmi leo baada ya kufikia makubaliano binafsi na mchezaji huyo

Mabingwa hao wa Ligi ya Mabingwa Afrika mara 10 walifikia makubaliano na Simba tangu wiki iliyopita na kilichobakia ilikuwa ni kumalizana na mchezaji huyo.

Usajili huo unampa nafasi Miquissone kufanya kazi kwa mara ya pili na kocha wa Al Ahly, Pitso Mosimane

Awali Miquissone alicheza chini ya Mosimane pindi kocha huyo alipokuwa akiinoa Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini ingawa hakumpa nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza

Mmoja wa viongozi wa Simba aliithibitishia Mwanaspoti Online kuwa dili la Miquissone limekamilika

"Miquissone ameuzwa rasmi kwa dau la Dola 900,000 na Banda (Peter) ndiye atakayeziba pengo lake. Ni suala la muda tu kabla ya klabu kutangaza rasmi. Inaweza kutangaza leo au kesho," alisema kiongozi huyo.