AKILI ZA KIJIWENI: Coastal wanapiga hela kwa akili

Muktasari:

  • Coastal ilivuna fedha hizo nyingi kwa vile Mwamnyeto alikuwa bado na mkataba umesalia wa kuitumikia timu hiyo kwa miaka miwili zaidi.

MWAKA 2020, Coastal Union ilipata fedha nyingi kupitia mauzo ya beki Bakari Mwamnyeto ambayo inakadiriwa kufikia takribani Sh 150 milioni.

Coastal ilivuna fedha hizo nyingi kwa vile Mwamnyeto alikuwa bado na mkataba umesalia wa kuitumikia timu hiyo kwa miaka miwili zaidi.

Kingine ambacho kilimfanya beki huyo wa kati kuwa lulu sokoni ni ushindani wa Yanga na Simba na Azam katika kuwania saini yake, timu ambazo zina nguvu kubwa kiuchumi.

Fedha ambazo Coastal Union ilipata kutokana na mauzo ya Mwamnyeto ndizo zilikuja kutumika katika kuimarisha kwa kiasi kikubwa kikosi chao kwa ajili ya msimu uliofuata.

Miaka minne baadaye kuna kiasi cha takribani Sh200 milioni kupitia mauzo ya beki wake tegemeo wa kati hivi sasa, Lameck Lawi ambaye ana umri wa miaka 18.

Safari hii ni timu mbili tu ambazo zinapigana vikumbo kuwania saini ya Lawi ambazo ni Simba na Azam na kila moja inatajwa kuwa tayari kutoa fedha ambazo Coastal wanazitaka ili kumuachia Lawi.

Kuna namna timu zinapaswa kujifunza kutoka kwa Coastal Union juu ya namna zinavyoweza

kutengeneza fedha nyingi kwenye soka nje ya zile za udhamini ambayo ni kupitia mauzo ya wachezaji.

Unaenda kutafuta vijana wenye vipaji mitaani au kwenye vikosi vya vijana, unawatengeneza na kuwafanya wawe bora kisha unawapa mikataba mirefu ambayo itakulinda pindi timu nyingine zinapowahitaji.

Hili wala halihitaji kutumia kiasi kikubwa cha fedha na badala yake ni kuwa na utulivu na mipango sahihi katika utekelezaji wake.