Ajibu: Samatta ametufungulia njia kucheza Ulaya

Muktasari:

Nahodha wa timu ya Taifa 'Taifa Stars' Mbwana Samatta jana amesaini mkataba wa miaka minne na nusu kuchezea klabu ya Aston Villa akitokea KRC Genk ya Ubelgiji.

Dar es Salaam.Siku moja baada ya nahodha wa timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars', Mbwana Samatta kusaini mkataba wa miaka minne na nusu katika timu ya Aston Villa nyota mbalimbali wa Ligi Kuu Tanzania Bara wamempongeza kwa hatua hiyo.

Wakizungumza na Mwanaspoti, kwa nyakati tofauti wachezaji hao walisema ni hatua kubwa aliyoipiga na amewafungulia milango na wao kupambana zaidi ili waweze kufikia mafanikio hayo aliyoyafikia mtanzania mwenzao.

Kiungo wa Simba, Ibrahim Ajibu amesema amestahili kupata nafasi kwenye timu hiyo kutokana na upambanaji wake ikiwa ni sambamba na malengo aliyokuwa amejipangia na kuongeza kuwa ni fulsa sasa kwao kupambana na wao wafuate nyayo zake.

"Hakuna kinachoshindikana ukiamua katika soka alipambana na kuzipambania timu alizoipita kitu kilichofanya aonekane zaidi nampongeza 'Popa' naamini ametufungulia njia sasa kila mmoja atapambana kwa nafasi yake kusaka nafasi ya kucheza huko," alisema Ajibu aliyekataa kujiunga na TP Mazembe mwanzoni mwa msimu huu.

Kipa wa Simba na Taifa Stars, Aishi Manula amesema ni heshima kwa nchi na wachezaji kwa ujumla bila kuwasahau watanzania wanaopenda soka kwa nahodha wao timu ya taifa kuliwakilisha taifa vizuri.

"Ni mwanzo mzuri amekuwa mfano wa kuigwa sasa kila mmoja atakuwa na nafasi ya kupambana zaidi ili aweze kufuata nyayo za Samatta, hongera sana na nakutakia kila lenye heri," alisema Manula.

Kipa wa Taifa Stars na KMC, Juma Kaseja amesema Samatta hajawahi kumuangusha wala kuliangusha Taifa hivyo anaamini atafanya mambo makubwa huko alikopata nafasi ya kucheza na kuyashawishi mataifa mengine kuja Tanzania kufuata vipaji.

"Nakutakia mafanikio yaliyomema nahodha umeanza wewe naamini wengine watafuata tuwakilishe vyema ili kuwapa nafasi viongozi wa timu nyingine kuja kusaka vipaji vilivyobaki umefungua milango wengi watafuata," alisema Kaseja.