Aggrey aagwa kwa heshima, Stars ikitoka sare na DR Congo
Timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' imemuaga Aggrey Morris kwa sare ya 1-1 dhidi ya DR Congo mchezo uliopigwa katika uwanja wa Benjamin Mkapa leo jioni.
Katika mchezo huo ambao uliambatana na kumuaga beki nguli wa Stars ana Azam, DR Congo ndio walikuwa wa kwanza kupata bao la kuongoza katika kipindi cha kwanza dakika 19 kupitia kwa Mayele Kalala mpaka dakika 45 za kwanza zinamalizika.
Kwenye dakika 45 za kipindi cha pili, kocha wa Stars, Etiene Ndayiragije aliamua kufunguka na kufanya mabadiliko.
Stars ilianza kwa kufanya mabadiliko ya kuwatoa Yassin Mustafa, Deus Kaseke na Adam Adam huku wakiingia Ditram Nchimbi, Yusuph Mhilu na Edward Manyama.
Edward Manyama alionyeshewa kadi ya njano baada ya kumfanyia madhambi Lilepo Makabi na kuwa faulo isiyokuwa na madhara.
Mabadiliko ya kwenye eneo la ushambuliaji yalionekana kuwa na tija kwani Nchimbi na Muhilu walikuwa wanatumia spidi zao kupeleka mashambulizi na kuwalazimisha mabeki wa DR Congo kufanya makosa.
Stars ilisawazisha dakika 51 kupitia kwa Ayoub Lyanga akionganisha kwa kichwa krosi ya Ditram Nchimbi.
Dakika 57 Stars walifanya mabadiliko mengine ya kumtoa Ayoub Lyanga na kuingia Farid Mussa.
Mabadiliko yote yalionekana kutaka kuongeza nguvu kwenye eneo la ushambuliaji na tija ilionekana kwani kuwa na washambuliaji wenye nguvu na spidi.
Dakika 78 Aishi Manula aliokoa shambulizi kwa mguu, baada ya winga wa DR Congo, Boka Isaka ambaye alipiga krosi ya chinichini ma kwenda ndani ya boksi la Stars.
Stars nao walijibu mapigo dakika 81 baada ya winga, Farid Mussa kupiga krosi na Ditram Nchimbi alionganisha huku mpira ukaenda mikononi mwa kipa wa DR Congo.
Dakika 84 Stars ilifanya mabadiliko ya kuwatoa Lucas Kikoti na Said Ndemla na nafasi zao zikichukuliwa na Israel Mwenda na Baraka Majogoro.
Wakati huo huo beki wa DR Congo, Kikasa Wamba alionyeshewa kadi ya njano baada ya kumfanyia madhambi Feisal Salum.
HESHIMA YA AGREY
Kabla ya timu hizo kuingia uwanjani, zilijipanga mstari, huku Agrey anayeagwa rasmi leo kutumika katika timu ya taifa akipita katikati.
Agrey alitangaza kustaafu kuitumikia timu ya Taifa ya Tanzania na Zanzibar pia mkataba wake Azam FC, ukimalizika ataacha kucheza.
ZAWADI ALIYOPEWA
Mbali na kuagwa kwa heshima, amepewa jezi, mpira na vyote vikisainiwa na wachezaji wote, viongozi na benchi la ufundi na hundi yenye thamani ya Milioni 5.
Hata hivyo amecheza dakika mbili kabla ya nafasi yake kuchukuliwa na Carol's Protasi.