Andaeni suti za ubingwa

PILAU la sherehe za ubingwa limeanza kupikwa. Wenye suti zao wameambiwa waziandae na wenye ndizi zao waziweke tayari. Kwa sababu Yanga imebakisha dakika 180 tu za uwanjani kukabidhiwa kombe lao na straika Fiston Mayele aliyerudi kwenye mbio za ufungaji jana amewaambia mashabiki; “Nimerudi, nitaendelea kufunga sikati tamaa mpaka tupate ubingwa.”

Wananchi jana walitakata. Walitawala kwa kila kitu kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa katika mechi ambayo kila mmoja aliosha nyota wakati wakiichakaza timu iliyo hatarini kushuka daraja ya Mbeya Kwanza kwa mabao 4-0.

Mayele, ambaye alikuwa hajafunga kwenye mechi nne mfululizo alitetema na kufikisha mabao 13. Saido Ntibazonkiza akafunga bao lake la saba la ligi msimu huu, Dickson Ambundo akatupia bao lake la pili mfululizo na Heritier Makambo aliwajaza kwa mara ya kwanza msimu huu. Ilikuwa ni raha tu kwa Wananchi, ambao ilikuwa ni mara yao ya pili msimu huu kutoa kipigo hicho kikubwa kwao baada ya awali kuifunga 4-0 Dodoma Jiji katika mechi yao ya raundi ya kwanza Desemba 21, 2021.

Saido ambaye sasa amehusika katika mabao 12 (kafunga 7, asisti 5), alikaribia kuifungia bao la tano Yanga jana katika dakika ya 90, lakini shuti lake la mbali liligonga nguzo ya lango la Mbeya Kwanza na kuokolewa.

Ushindi umeifanya Yanga kufikisha pointi 63 na inahitaji pointi 6 nyingine katika mechi zao mbili zijazo dhidi ya Biashara United Jumanne jijini Mwanza na Coastal Union Kwa Mkapa Juni 15 kutwaa taji lao la 28. Kocha wa Yanga, Nabi Mohammed alisema; “Tulicheza kimkakati na tumepata tulichokuwa tunakitaka, tucheza kwa malengo mpaka dakika ya mwisho.” Mayele yeye alisisitiza kwamba alijua atafunga kutokana na mzuka aliokuwa nao.


USAJILI

Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano na Usajili wa Yanga, Hersi Said ametamba kwamba watashusha vyuma vya maana kwenye usajili unaoanza hivi punde na hawakuwahi kufeli kwenye ishu ya usajili. Msimu uliopita Hersi alinyooshewa vidole kwa usajili alioufanya wa mastaa Carlos Carlinhos, Michael Sarpong, Fiston Abdulrazaq ambao walishindwa kuisaidia timu na kuondolewa katika orodha ya nyota wa msimu huu.


Yanga; Djigui Diarra, Kibwana Shomari, Farid Mussa/ Yassin Mustafa, Yanick Bangala, Dickson Job, Khalid Aucho/ Zawadi Mauya, Salum Abubakar ‘Sure Boy’, Jesus Moloko, Dickson Ambundo/ Chico Ushindi, Said Ntibazonkiza na Fiston Mayele/ Heritier Makambo.

Mbeya Kwanza; Hamad Kadedi, Mizar Kristom, Salumu Chuku, Jofu Wilson, Rolland Msonjo, Joseph Majagi, Jimmy Shoji, Chesco Mwasimba, Habib Kiyombo, Eliuter Mpepo na Fredrick Magata.