Prime
Ujenzi uwanja wa Yanga Jangwani kiza kinene
LEO Jumapili ni siku ya 100 kamili tangu Yanga ilipokabidhiwa hati ya ongezekeo la ardhi kwa ajili ya ujenzi wa Uwanja wa Yanga pale makao makuu ya klabu hiyo.
Kama umesahau, Yanga ilikabidhiwa hati hiyo Septemba 12 mwaka huu katika tamasha la saba ya Kilele cha Siku ya Mwananchi lililofanyika kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Hati hiyo ilikabidhiwa na aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Deogratius Ndejembi baada ya kuwaahidi Wanayanga wenzake kupitia mkutano mkuu wa mwaka uliofanyika Septemba 7 kwamba ndani ya wiki mbili tu angewapatia hadi na kuiwahisha mapema zaidi.
Mbele ya mashabiki walioujaza Uwanja wa Mkapa, mabosi wa klabu hiyo uliutangazia umma kuwa, lile ombi lao la kuongezewa eneo pale yalipo makao makuu ya klabu hiyo limepita na kukamilika.
Katika hafla ya Kilele cha Wiki ya Mwananchi, Waziri Ndejembi ambaye kwa sasa ni Waziri wa Nishati, alikabidhi hati ya ongezeko la eneo hilo kutoka Wizara ya Ardhi kwa Rais wa klabu hiyo Injinia Hersi Said, huku mashabiki na wanachama wake wakifurahia hatua hiyo.
Ukabidhiwaji wa hati hiyo ulikuwa ni kama muendelezo wa ndoto inayoishi ndani ya kichwa cha shabiki au mwanachama yeyote wa Yanga kwamba enzi za klabu yao kumiliki uwanja wake zinakuja na kuna hatua imepigwa kwa kipengele hicho kuondoshwa na serikali.
Ikumbukwe kwamba Yanga hapo Jangwani iliwahi kumiliki uwanja uliokuwa ukitumika kwa mazoezi ya klabu za timu hiyo na hata mechi za kirafiki uliofahamika kwa jina la Uwanja wa Kaunda, lakini baadaye kutokana na shida ya kufurika kwa mto Msimbazi uliharibu uwanja huo.
Kiu ya mashabiki wengi wa Yanga ni kutamani kuona klabu yao siku moja inarudisha heshima yake ya kuwa klabu kongwe ikicheza mechi zake au baadhi kwenye uwanja wao wenyewe na sio vile viwanja vya kukodi kila wakati.
Hata hivyo, jana Desemba 21 lilitimia kikamlifu siku 100 tangu Yanga ikabidhiwe hati hiyo ambayo ilikuwa ombi la uongozi wa klabu hiyo kwamba kama ikipata ruhusa hiyo basi hatua muhimu za kwenda kuujenga uwanja wao zinakwenda kutimia.
Wakati siku 100 zinatimia ambazo ukizichambua inakuwa ni miezi mitatu na siku 10 bado hakuna dalili ya wazi katika eneo hilo au hata nje zilizoonyesha kwamba au kutangazwa kwamba harakati ya ujenzi wa uwanja huo zinaendelea.
KINACHOFANYIKA JANGWANI
Ndani ya siku 98 Mwanaspoti limepita eneo la Jangwani na kukuta bado hali iko vilevile, likiwa ni eneo la wazi ambalo limesawazishwa kama ambavyo ilikuwa kabla ya kukabidhiwa hati hiyo huku shughuli nyingine za kibinadamu zikiendelea.
MAEGESHO YA MAGARI
Ukifika eneo hilo la Jangwani linalomilikiwa na Yanga utakuta shughuli kubwa zinazoendelea pale ni eneo hilo kugeuzwa maegesho ya magari ya watu mbalimbali wanaokwenda Kariakoo na maeneo mengine, ambapo ukifika hapo unapokewa na walinzi maalumu wanaochukua fedha kwa watu wanaoegesha magari eneo hilo.
KIBANDA CHA KAHAWA
Lipo eneo ambalo kuna banda la watu mbalimbali kupata kahawa ambapo hapo utawakuta mashabiki na wanachama wa Yanga wakipiga stori za mambo kuhusu klabu yao lakini pia mambo ya taarifa mbalimbali za soka.
MATEJA NAO
Wale jamaa wanaoaminika kutumia dawa za kulevya maarufu kama mateja, nao bado wanaonekana wakijificha pembezoni mwa eneo wakipata burudani zao huku wakifanya kwa akili kuwakimbia watu na walinzi ambao wanalinda jengo hilo.
BAADHI HAWAJAHAMA
Eneo ambalo Yanga iliongezewa litawalazimisha baadhi ya watu waliokuwa wanafanya shughuli zao kuhama, lakini mpaka wakati ambao Mwanaspoti ilipofanya ziara ya siri, baadhi ya watu hao bado walikuwa wanaendelea na shughuli zao kama ambavyo ilikuwa kabla.
MKWARA WA MCHENGERWA
Wakati Yanga ikiwasilisha maombi ya eneo hilo la nyongeza lilitua kwa aliyekuwa Waziri wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Mohammed Mchengerwa, aliyewahi kuupiga mkwara uongozi wa Yanga kwamba endapo serikali itapitisha maombi hayo kisha wasipofanya chochote, uamuzi mwingine unaweza kuchukuliwa huku akiwasisitiza viongozi wa klabu hiyo kufanya kweli.
DENI KITANZI CHA HERSI
Injinia Hersi amefanya makubwa katika uongozi wake ndani ya klabu hiyo, akielekea kumaliza muhula wake wa kwanza, lakini kama kuna deni ambalo amelibakisha basi ni kukamilika kwa ahadi hiyo ya ujenzi wa uwanja wa klabu hiyo.
Ikumbukwe Yanga ilishatangaza kwamba mfadhili wao Ghalib Said Mohammed ‘GSM’ ndiye mbeba maono kwenye harakati za ujenzi wa uwanja huo ambapo mchakato huo utasimamiwa na tajiri huyo ambaye amefanya makubwa kwenye kuirudishia ubabe klabu hiyo.