Kwaheri Goncalves, Yanga ijitathmini
Muktasari:
- Anakuwa Kocha Mkuu wa tano kuachana na Yanga ndani ya misimu miwili ya hivi karibuni akifuata nyayo za Romain Folz, Miloud Hamdi, Sead Ramovic na Miguel Gamondi.
GHAFLA tu Yanga imeamua kuachana na Kocha Mkuu wake Pedro Goncalves huku timu hiyo ikiwa inaongoza msimamo wa Ligi Kuu.
Anakuwa Kocha Mkuu wa tano kuachana na Yanga ndani ya misimu miwili ya hivi karibuni akifuata nyayo za Romain Folz, Miloud Hamdi, Sead Ramovic na Miguel Gamondi.
Kati ya makocha hao watano, ni Ramovic pekee ambaye aliachana na timu hiyo kwa uamuzi wake binafsi na siyo klabu iliamua kuachana naye lakini wengine wanne waliobakia, wote walionyeshwa mlango wa kutokea na Yanga.
Makocha hao wote waliachana na Yanga huku timu hiyo ikiwa bado katika mwenendo mzuri kwenye Ligi Kuu na mashindano mengine lakini sababu kubwa inayotajwa kuwa chanzo cha kuondolewa kwao ni timu kutoonyesha kiwango cha kuvutia.
Hapa kijiweni tunaheshimu uamuzi ambao umekuwa ukifanywa na uongozi wa Yanga wa kuachana na makocha wao lakini tunashauri baada ya kuondoka kwa Goncalves, klabu inapaswa kujifanyia tathmini.
Idadi ya makocha wakuu watano katika misimu miwili huku pia kukiwa na makocha wengine wawili tofauti waliokaimu nafasi, sio ndogo na inaonyesha tatizo halipo katika benchi la ufundi pekee bali na maeneo mengine.
Inawezekana kuna tatizo pia upande wa wachezaji katika kufanyia kazi kile ambacho wanaelekezwa na benchi la ufundi wakakitimize ndani ya uwanja katika michezo husika.
Pia mashabiki ambao wamekuwa wakichangia kwa kiasi kikubwa kuweka presha inayosababisha makocha hao kuondolewa, wanatakiwa wafahamu, jambo kubwa na la msingi katika timu ni kupata matokeo mazuri na siyo mara zote timu itacheza kandanda la kuvutia.
Inawezekana timu haiathiriki ndani ya uwanja kutokana na mabadiliko hayo ya makocha lakini kuna hasara inayoingia katika kulipa fidia za kuvunja mikataba.