Changamoto za As Vita na Ibenge Afrika

HAKUNA ubishi As Vita kwa sasa wanapitia katika mazingira magumu zaidi na hii imemfanya hata kocha wa timu hiyo, Florent Ibenge aumize kichwa anapokuwa na mchezo wowote.

AS Vita ya msimu huu sio ile ya misimu miwili iliyopita iliyokuwa ikitoa changamoto kubwa kwa baadhi ya timu vigogo wa Afrika.

Mwanaspoti linakuletea mambo yaliyochangia timu hiyo iyumbe na kutaka kuondoka katika orodha ya timu tishio Afrika.


BOSI MPYA BADO BADO

AS Vita kwa sasa ipo chini ya rais mpya, mwanamama Bestine Kazadi baada ya kushinda kwenye uchaguzi wao na bado hajaweza kuiongoza vizuri timu hasa kwenye maamuzi yake ya kiutendaji.


KUYUMBA KIUCHUMI

Kwa sasa As Vita haipo vizuri sana kiuchumi na imechangia kushindwa kupambana na timu zenye pesa.

Imeuza mastaa wake mbalimbali kama Tonombe Mukoko, Tuisila Kisinda na Jean Makusu na haijapata warithi wao sahihi.

Hilo ni kama pigo kwao kwani walikuwa wanahitaji pesa lakini walishindwa kutengeneza wachezaji wengine na kutumia vijana huku wakisahau wanakabiliwa na mashindano ya Ligi ya Mabingwa na wanakutana na timu ngumu zenye nyota wenye viwango vya juu.

Usajili pekee iliyofanya ni wa Papy Tshishimbi aliyemaliza mkataba Yanga msimu uliopita na ikitumia na vijana imejikuta ikitumia nguvu kubwa kwenye kupata matokeo tofauti na misimu miwili iliyopita.


PRESHA KUBWA KWA IBENGE

Ibenge ana presha kubwa kuanzia upande wa klabu pamoja na timu ya Taifa ya DR Congo.

Kocha huyu ni miongoni mwa makocha wanaounda benchi la ufundi la timu ya Taifa na kwa matokeo wanayoyapata kipindi hiki sio mazuri hivyo lazima awe na presha.

Presha hiyo inamfanya afanye kazi yake katika kiwango cha kawaida kwani anakosa kujiamini na kujigawa vizuri pande mbili.

Kwa upande wa wenzake wa TP Mazembe wanaonekana kugawana majukumu vizuri kwa kupeana nafasi tofauti na yeye kila sehemu anataka kusimama mwenyewe.