Wanawake bora kwa Diamond ni Zari na Wema

Muktasari:

Inaelezwa sifa kuu ya Wema kujua kupika halikadhalika na Zari, hivi ni kigezo vinavyowafanya kuwa wanawake bora kwa Diamond.

 

KITENDAWILI cha kijembe cha nani hasa alikuwa anaambiwa kuwa huwa hampikii Diamond kimeteguliwa na Esma ambaye ni dada wa msanii Diamond Platnumz.

Hatua hiyo inakuja ikiwa ni siku chache tangu Esma aandike kijembe kwenye ukurasa wake wa mtandao wa Instagram kumsifia Zari.

Esma aliweka picha ya Zari aliyovalia gauni jeupe huku mkononi akiwa ameshika chupa ya shampeni na kuandika "Ila nisiwe mnafiki nachompendea Zari kaingia kwenye friji kaona haelewi kawatuma kina dada sokoni wakanunue vitu kwaajili ya kuingia jikoni ajipikie chakula fresh cha watoto wake.

“Ila Diamond shavu utapata mpaka aondoke sio vile videmu vyako vinavyokuleteaga vichips na nikija nikiviona tena nitavifukuza na mkia wa taa. Ulipo nipo ila sitaki wa kuleta vichips,”aliandika Esma.

Zari alitua nchini Alhamisi Novemba 5, 2020 na watoto wake Tiffah na Nillan, na tangu siku hiyo ameweza kuteka mitandao ya kijamii vilivyo kwa watu kufuatilia mambo wanayoyafanya. Ambapo moja ya video iliyotrendi ni kuonekana  yupo jikoni anapika.

Akihojiwa  na kituo cha televisheni cha Wasafi, waliotaka kujua kijembe kile kilikuwa cha nani, alikwepa kumsema moja kwa moja lakini alijikuta akifunguka hilo baada ya kuulizwa kati ya wanawake ambao kaka yake amewahi kuwa nao kwenye mahusiano nani anamuona ni bora ni kwa nini.

Baadhi ya wanawake ambao Diamond amewahi kuwa nao  katika mahusiano  na kujulikana waziwazi ni pamoja na Wema Sepetu, Penny.

Wengine ni  Zari, mwanamitindo Hamisa Mobeto na Tanasha Dona ambao hawa amezaa nao watoto wa kiume.

Dada huyo katika majibu yake aliwataja wanawake bora kuwa ni Zari na Wema na kutaja sababu kuwa ni kutokana na kumjali ikiwemo kumpikia, tofauti na wanawake wengine.

“Yaani Zari na Wema ni wanawake ambao wanajali mwanaume wao kwa kula, na siku zote ili mwanaume apate nuru, apate shavu ni kula, si mwanaume unamletea chips.

"Maana utasikia watu wanachamba kuwa ooh! Wee mwenyewe ndoa yako imekushinda, muite mume wangu hapa atakuhadithia kuhusu suala la kumjali kwenye kula,” amesema Esma.