Ujauzito wa Vanessa wampaisha Jux

Ujauzito wa Vanessa wampaisha Jux. Hivyo ndivyo  unavyoweza kusema baada ya wimbo wake wa  ‘Sina Neno’ kutrend namba tatu.
Wimbo huo aliutoa siku moja baada ya Vanessa kuanika ujauzito wake.
Septemba 7, Jux na mchumba wake Rotimi katika kurasa zao za mitandao ya kijamii waliweka  picha zikimuonyesha Vanessa kuwa mjamzito na kueleza kuwa wanatarajia kupata mtoto wa kiume siku za usoni.
Vanessa na Jux wamewahi kuwa katika mahusino kwa muda mrefu na baada ya kuachana, mrembo huyo aliangukia mikononi mwa mwigizaji na mwimbaji Rotimi, raia wa Nigeria mwenye makazi yake nchini Marekani.
Hata hivyo mara baada ya kuonesha ujauzito, baadhi ya watu walimpiga vijembe Jux, huku wengine wakienda mbali zaidi na kueleza kuwa mkali huyo wa kibao cha ‘Sisikii’ atakuwa anajisikia vibaya.
Katika kuonyesha kuwa wala sivyo watu wanavyowaza, Jux kaamua kujibu kizungu kwa kutoa wimbo huo wa ‘Sina Neno’, wimbo ambao mpaka sasa umeshatazamwa zaidi na watu laki nane.
Moja ya kibwagizo katika wimbo huo ni “Niko salama,mimi sina neno,utaitwa mama mtoto  mpe upendo,”.
Pia katika kunyesha anaikubali couple hiyo, Jux katika wimbo huo kuna mahali anaimba”Mnapendezana na pendo liko kasi kasi, mkipostiana Instagram Status, tushafunika kurasa mambo ya zamani yalishapita,”.
Kizuri zaidi ni vile alivyomalizia wimbo huo kwa kuweka sauti ya mtoto akilia.