TUONGEE KISHKAJI: Wasanii tunawaponda ila wako vizuri kimtindo

KUSEMA ukweli washkaji, tunaweza kukaa kijiweni siku nzima tukimponda Alikiba. Wengine tuseme anajibebesha ufalme wa bure lakini wala sio taji lake hilo, yaani kama ingekuwa viatu tungesema vinampwaya. Wengine tuseme anafanya muziki kiujanjaujanja. Si umesikia kuna wimbo kwenye albamu yake mpya ya Only One King unadaiwa kuwa umeibwa kwa msanii chipukizi.

Kisha tuhamie kwa Mondi tuseme huyo ndo kaisha kabisa. Ngoma zake hazina mvuto siku hizi. Anaimba matusi matupu, kwanza wala hazisumbui mtaani hadi azibusti na kiki za mademu. Mara oooh wimbo huu unanikumbusha nilivyokuwa na Wema Sepetu, mara Zari hivi, mara Tanasha vile blaaah! blaaah! nyingiiii.

Kisha tuhamie kwa Nandy, Zuchu, Marioo na Idris Sultan halafu Harmonize na Konde Gang yake yote.

Maua Sama, Young Lunya, Jay Melody, Vicent Kigosi na wasanii wote waliopo kwenye gemu sasa hivi, bado haitafuta ukweli kwamba hivyo vichwa sio vya kawaida, ni wapambanaji. Wamepiga hatua kubwa na kimtindo fulani wanastahili pongezi zao.

Diamond anayeitwa bosi na kila mtu leo hajamaliza hata kidato cha nne. Kama kasoma sana basi kaishia kidato cha pili. Lakini tazama mambo aliyoifanyia Tanzania. Tazama jinsi alivyobadilisha jina la familia yake kutoka kifamilia fulani tu pale Tandale ambayo muda mwingine ilikuwa inapiga deshi, yaani mchana unapita hakipikwi kitu hadi kuwa taasisi kubwa. Sasa hivi mama yake ana tubiashara twa kueleweka mjini. Dada zake wana mishe. Kaka zake wana mitikasi yao. Wadogo zake wana mishe. Kila mtu yuko sawa. Hiyo ni hatua ya kupongezwa. Usichukulie poa kuwa mtu ambaye unakata mzizi wa umasikini kwenye familia yako.

Marioo mnayemuona leo anawaimbisha Bia Tamu klabu, ana gari nzuri. Anaishi kwenye nyumba nzuri. Ana uhakika wa kula na kuvaa vizuri. Watoto wakali wanamshobokea hakuwa hivyo miaka saba nyuma. Picha linaanza alikuwa analelewa na bibi yake -tena bibi choka mbaya, labda choka mbaya sio jina zuri

lakini huo ndi

yo ukweli, mwenyewe anasema walikuwa hata wanaishi nyumba ya udongo na hakuna mswahili anayeishi kwenye nyumba hizo kwa kupenda, ni maisha tu.

Wajomba wakamchukua wakamtupa gereji kama madogo wengi kwenye familia zetu wanavyosukumiwa huko wakionekana wapo wapo.

Mwenyewe anakwambia kaenda gereji katoka kama alivyoingia, hajui ‘gear box’ hajui lolote. Lakini leo hii anaishi kwenye maisha ambayo pengine hakuwahi hata kuamini kama yanaweza kutokea, kimtindo fulani unaweza kusema amekata ile harufu ya kupigika ya familia yao, hiyo sio kitu cha kawaida mshikaji wangu.

Ni kweli tukiwa vijiweni inanoga sana kuongelea wasanii, lakini tufanye kama burudani ili kuchangamsha genge lakini tuache nafasi ya ukweli kwamba hawa washikaji tunawaponda ila kimtindo wako vizuri.