Rayvanny aweka macho kwa Rose Muhando
Muktasari:
- Akizungumza na Mwanaspoti, Rayvanny amesema licha ya wao kuwakilisha mitindo tofauti ya muziki, jambo hilo halimzuii kuona uwezekano wa kushirikiana na Rose Muhando katika kazi itakayobeba ujumbe wenye manufaa kwa jamii.
STAA wa muziki wa Bongo Fleva, Rayvanny ameweka wazi kuvutiwa na mkongwe wa muziki wa Injili, Rose Muhando, kufuatia kukutana kwao jijini Dodoma katika viwanja vya Bunge, huku akieleza kuwa angependa siku moja kufanya naye kazi.
Akizungumza na Mwanaspoti, Rayvanny amesema licha ya wao kuwakilisha mitindo tofauti ya muziki, jambo hilo halimzuii kuona uwezekano wa kushirikiana na Rose Muhando katika kazi itakayobeba ujumbe wenye manufaa kwa jamii.
“Rose Muhando ni msanii mkubwa sana kwenye Gospel (Injili), namuheshimu sana. Kukutana naye kunanipa hamasa ya kufikiria kitu cha pamoja siku moja,” amesema Rayvanny.
Kauli hiyo imekuja wakati Rose Muhando akiendelea kubaki miongoni mwa wasanii wa Injili waliowahi kufanya kazi na wasanii kutoka maeneo tofauti, jambo lililomfanya kujijengea nafasi ya kipekee ndani na nje ya Tanzania.
Kwa upande wake, Rose Muhando ameliambia Mwanaspoti kuwa, hana tatizo kufanya kazi na msanii yeyote wa Bongo Fleva ilimradi kazi husika iwe na ujumbe mzuri unaolenga kujenga maadili na kuleta mabadiliko chanya katika jamii.
“Mimi sina tatizo kufanya kazi na msanii yeyote, iwe Bongo Fleva au Gospel, kikubwa ujumbe uwe mzuri na wenye kujenga jamii,” amesema Rose Muhando.
Kwa mujibu wa kauli za wasanii hao, wazo la kufanya kazi pamoja linaonekana kupata mwanga, jambo linalofungua uwezekano wa kuwakutanisha kwenye mradi mmoja wa muziki hapo baadaye.