Polisi: Hatuna taarifa ya ajali ya Shilole, wamuita
Muktasari:
- Mapema jana asubuhi Mbunge wa Kigoma Mjini, Baba Levo aliandila kupitia akaunti zake za mitandao ya kijamii akisema Shilole alipata ajali kwa kugonga ng'ombe.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Kigoma limetoa ufafanuzi wa taarifa inayosamba katika mitandao wa kijamii ikidai msanii wa muziki, Shilole kupata ajali ya gari na kujeruhiwa akiwa safarini akitokea mkoani Kigoma kwenda jijini Dodoma, ambapo gari aliyokuwa akiitumia kwa safari aina ya Toyota Alphad ambayo namba zake za usajili bado hazijafamika iligonga ng'ombe eneo la Maragalasi wilayani Uvinza.
Katika taarifa hiyo ya Polisi inasomeka; "Ukweli ni kwamba taarifa hiyo ya ajali haijaripotiwa kituo chochote cha Polisi Mkoa wa Kigoma, hata hivyo tunashauri dereva yeyote anapopata ajali akiwa safarini ambayo imepelekea kifo, majeruhi au uharibifu wa chombo ana wajibu wa kutoa taarifa kituo cha Polisi ili aweze kupata msaada wa matibabu, kuchunguza chanzo cha ajali na kuchukua hatua stahiki za kisheria kwa mtuhumiwa."
Taarifa hiyo inaongeza; "Polisi wametoa wito kwa Shilole kufika kituo chochote cha polisi kuripoti ajali hiyo, ili uchunguzi uweze kufanyika na hatua stahiki za kisheria ziweze kuchukuliwa kwa mtuhumiwa aliyesababisha ajali hiyo."
Pia jeshi hilo Mkoa wa Kigoma limewataka madereva wa vyombo vya moto mkoani humo kuendelea kutii na kufuata sheria za usalama barabarani, ili kuepuka ajali ambazo zinaweza kutokea kutokana na uzembe wa madereva.
Mapema jana asubuhi Mbunge wa Kigoma Mjini, Baba Levo aliandila kupitia akaunti zake za mitandao ya kijamii akisema Shilole alipata ajali kwa kugonga ng'ombe ambapo watu mbalimbali walitoa maoni yao, baadhi wakimpa pole na wengine wakitoa kejeli wakiuliza afya na usalama wa ng'ombe.