Babalevo aelezea ajali ya Shilole
Muktasari:
- Akizungumza na Mwanaspoti, Mbunge wa Kigoma Mjini Baba Levo amesema, Shilole amepata ajali mbaya hivyo anahitaji maombi apone haraka.
Msanii wa muziki Zuwena Mohammed maarufu kama Shilole amepata ajali ya gari akiwa njiani kwenda Dodoma kutoka mkoani Kigoma, alikokuwa ameshiriki katika shughuli ya kijamii iliyoandaliwa na Mbunge wa Jimbo la Kigoma Mjini Clayton Revocatus (Babalevo), iliyojulikana kama Pilau Day.
Akizungumza na Mwanaspoti, Mbunge wa Kigoma Mjini Baba Levo amesema, Shilole amepata ajali mbaya hivyo anahitaji maombi apone haraka.
"Ni kweli Shilole amepata ajali, anahitaji maombi apone haraka, anaendelea kupata matibabu Tabora," amesema.
Aidha kupitia ukurasa wake wa mitandao ya kijamii wa Instagram, Baba Levo amethibitisha tukio hilo akisema: “Jana usiku dada yangu Shilole alipokuwa anatoka Kigoma kurudi Dodoma alipata ajali ya gari aina ya Alphard baada ya kugonga ng’ombe maeneo ya Maragalasi. Tunafuatilia afya yake kwa ukaribu, kwa sasa anaendelea kupata matibabu Tabora.”
Mwanaspoti linaendelea kufuatilia zaidi, usikae mbali.