MUSIC FACTS: Kitabu cha Wema Sepetu katika Bongo Fleva

BAADA ya kukabidhi taji la Miss Tanzania aliloshinda mwaka 2006, Wema Sepetu alieleka nchini Malaysia aliposomea Biashara ya Kimataifa katika Chuo Kikuu cha Limkokwing, akiwa huko ndipo filamu yake ya kwanza, A Point of No Return ilipotoka.

Tangu wakati huo Wema amefanya mengi katika filamu lakini pia kwenye muziki wa Bongofleva jina la Wema limechukua nafasi kubwa na yeye kuna baadhi ya vitu amefanya upande huo. Bongo Music Facts inakujuza zaidi;


1. Wema anaamini hawezi kuimba ila anaweza kuingiza sauti za chini (back vocal) katika wimbo wowote ule na amekuwa akifanya hivyo kwa miaka mingi ila ni nyimbo chache zinazofahamika kwa sababu sio jambo analolipa sana nafasi.


2. Chini ya kampuni yake, Endless Fame, Wema alifungua lebo ya muziki, Endless Fame Label (2016) na kuwasaini wasanii wawili, Mirror na Ally Luna, hata hivyo, mradi huu ulikuja kuishia njiani.

Ukiachana na Wema, wasanii wa kike Bongo ambao wana lebo zao ni pamoja na Vanessa Mdee (Mdee Music), Shaa (SK Music), Nandy (The African Princess), Shilole (Shishi Gang), Hamisa Mobetto (Mobetto Music) n.k.


3. Wema ndiye ameingiza sauti za chini katika wimbo wa Haitham Kim ‘Play Boy’ ambao ulifanya vizuri kwa kiasi chake, ni wakati ambao Haithm Kim akiwa chini ya MJ Records.

Naye Haitham Kim amefanya kitu kama hicho katika nyimbo kama Freedom wake Sugu, Kila Wakati wa Godzilla, Migulu Pande wa Madee na Fundi wake Mhe. Temba.


4. Wimbo wa Mr. Blue ‘Roho Inauma’ aliuandika maalumu kwa ajili ya Wema kipindi wakiwa na uhusiano ulioanza baada ya Wema kutwaa taji la Miss Tanzania, kipindi hicho Blue alikuwa maarufu Bongo kuliko Wema.

Utakumbuka pia ngoma ya Mr. Blue, ‘Baki na Mimi’ ameiandika kwa ajili ya mke wake, Waheeda ambaye kwa mara ya kwanza walikutana Club Bilicanas, Dar es Salaam, na tayari wana watoto watatu.


5. Gosby ndiye msanii wa kwanza wa Rapa Bongo kutoa wimbo unaoitwa Wema, ulitoka Novemba 2014 na unapatiikana kwenye mixtape yake iitwayo Miss Tape.

Huyu ndiye msanii wa kwanza Tanzania kutumia Vevo ni Gosby ambapo Aprili 28, 2015 aliweka wimbo wake, B.M.S (Baby Making Swag).


6. TID aliandika wimbo wake ‘Nilikataa’ akimshirikisha Mr. Blue na Q Chief kwa lengo la kutoa ya moyoni baada ya kupigwa chini na Wema aliyekuwa mpenzi wake na kumfanya kuwa mtu mwingine kabisa kitabia.

Kuwa na Wema kulimfanya TID kuandikwa sana na magazeti ya udaku kitu ambacho hakukipenda na kilimuumiza sana ila ilimbidi akubaliane nacho kwa wakati huo.


7. Alikiba, Diamond na Harmonize wamewahi kumuimba Wema katika nyimbo zao, Alikiba kupitia wimbo wake ‘Aje’, Harmonize kupitia ngoma yake ‘Mtaje’ na Diamond kupitia nyimbo zake mbili, Kesho na Fire akimshirikisha Tiwa Savage kutokea Nigeria.


8. Wema ndiye mtu wa kwanza kumpa Lulu Diva kazi ya video vixen ambapo alitokea kwenye video ya wimbo wa msanii wa Endless Fame Label, Mirror, Naogopa.

Ni Lulu Diva aliyewahi kuingia kwenye mchakato wa kuwania Miss Tanzania, alishinda kuwa Miss Kibaha kisha Miss Pwani, ila alishindwa kuendelea mbele kufuatia kifo cha baba yake mzazi.


9. Kati ya warembo watano waliongia tano bora ya Miss Tanzania mwaka 2006, watatu kati yao ambao ni Wema, Jokate Mwegelo na Irene Uwoya wameitumika sana Bongofleva ikiwa ni pamoja kutokea kwenye video za nyimbo za wasanii.


10. Wema ameingiza sauti za chini katika nyimbo mbili za Diamond Platnumz, Chanda Chema na Lala Salama uliobeba jina la albamu yake ya pili iliyotoka mwaka 2012 ikiwa na nyimbo 10.

Utakumbuka Hamisa Mobetto pia amefanya kitu kama hicho katika wimbo wa Diamond ‘Nikifa Kesho’, ni kabla hata hajatoa wimbo wake wowote ule na hadi sasa wawili hao ambao waliwahi kuwa wapenzi wameshirikiana kwenye nyimbo mbili.