Nakshinakshi taarab hawajamaliza

BAADA ya bendi yao kuachia mkwaju mpya wiki hii, mkurugenzi na msanii wa Bendi ya Taarab ya Nakshi Nakshi Father Mauji, amewahakikishia mashabiki mikwaju mingi zaidi iko njiani na itaachiwa hivi karibuni kwa mpigo.

Akizungumza na Mwanaspoti, mtaalamu huyo wa kucharaza gita la solo ambaye pia aliwahi kupiga katika bendi ya Jahazi Mordern Taarab ya Mzee Yusuph, amesema mbali na wimbo walioachia tarehe 4 unaoitwa Waja Mna Nongwa ulioimbwa na Farida Kindamba (pichani chini), bendi yake wamesharekodi ngoma zaidi ya tatu, wanachosubiri ni kuziachia tu.

“Baada ya hii tuna nyimbo tatu ziko tayari, tunasubiri siku ya kuziachia tu. Tunamalizia mazungumzo na menejimenti tujue itakuwa lini na lini, lakini plan ni kwamba tutakuwa tunaachia angalau wimbo mmoja kila mwezi ili zipeane nafasi,” ameeleza Father Mauji.

Akizitaja ngoma hizo kwa majina (majina ya walioimba kwenye mabano) amesema ni; Usifosi Kupendwa (Amina Mnyalu), Niondoshee (Mwasiti Kitoronto) na Mungu Hajaribiwi (Aisha Mtamu Kabisa).

Uzinduzi wa wimbo wa Waja Mna Nongwa utafanyika Oktoba 18 katika ukumbi wa Ikweta Grill, Kwa Aziz Ally Dar es Salaam.