Man Fongo afichua siri za Ma-Dj wa uswazi

MKALI wa miondoko ya singeli, Aman Fongo 'Man Fongo' amefichua siri zake za kupenda kuwatumia Madj wa uswahili katika shoo zake, akidai ufahamu wao wa mambo ya uswahili ndio unaowabeba!
Akizungumza na Mwanaspoti mapema leo, Man Fongo amesema matumizi ya madj hao hayapo kwake tu, bali ni wasanii karibu wote wa singeli nchini  wakipanda jukwaani huwa wanataka ile asilia ya  singeli inayotoka uswahilini yaani  Dj huwa anatengeneza kitu palepale na kuwapa mzuka mashabiki sambamba na waimbaji.
Man Fongo, amesema hii imekaa tofauti na Madj wengine ambao hawaujui mambo ya uswahili na ukiwachukua wanapiga nyimbo zilizorekodiwa kabisa, bila kuweka viel vionjo vinavyowapa mzuka mashabiki.
"Hili swali watu wengi huwa wanajiuliza kwanini wasanii wa singeli hupenda kuwatumia Madj wao wa uswahilini, hii ni kutokana na  waimbaji wa miondoko hiyo wakipanda jukwaani wanataka uasili kabisa wa singeli linapotoka uswahilini yaani tunakuwa kama tunapiga live shoo." amesema na kuongeza;
"DJ akisimama huwa anapiga live, yaani akitengeneza kitu pale mimi ndio ananipa mzuka palepale na mizuka ya palepale nae anapata kitu cha kutengeza pale pale ndio maana tunaweka madj wetu. Sio kwamba Madj wengine hawawezi, ila wao wanasimamia misingi yao ya kupiga  zile nyimbo zilizorekodiwa kabisa ambazo hazina mzuka sana jukwaani," amesema staa  Hainaga Ushemeji na ngoma nyingine kadhaa kama Hauna, Yeye na Sio Poa.