Diamond: Eto’o, Drogba wamenishauri niwekeza katika soka

Muktasari:

Mwanamuziki huyo amesema mchakato huo umeanza kitambo akiwashirikisha nguli wa soka Afrika, Samwel Eto’o na Didier Drogba.

Dar es Salaam. Mwanamuziki Diamond Platinumz, amesema ana mpango wa kuwekeza katika soka kwa kuanza harakati kuwatafutia timu nje ya nchi vijana wenye vipaji vya soka nchini.

Mwanamuziki huyo amesema mchakato huo umeanza kitambo akiwashirikisha nguli wa soka Afrika, Samwel Eto’o na Didier Drogba.

Akizungumza wakati akitambulishwa kuwa balozi wa Pari Match Tanzania, Diamond alisema menejiment yake imekuwa na plani ya kuingia katika soka.

"Sikutaka kuisema hii, lakini kwa muda mrefu zaidi ya mwaka mmoja na nusu tumekuwa na wazo hilo ambalo niliwashirikisha Eto’o na Drogba.

Alisema alishauriwa kununua nyumba Ufaransa ili kuwa na kituo maalumu cha kufanikisha mchakato huo.

"Nimeanza kutafuta nyumba Ufaransa, nimemshirikisha Drogba kwenye hilo na siku si nyingi zoezi litaanza," alisema Diamond

Alisema Eto’o amemshauri njia bora ya kuwekeza katika soka jambo ambalo alitamani kulifanya muda mrefu.

Akizungumzia nafasi ya kuwa balozi wa Pari Match Tanzania ambayo ni kampuni ya michezo ya kubashiri, Diamond alisema kabla ya kuingia mkataba na kampuni hiyo aliichunguza na kutambua umuhimu wake.

"Sikutaka kuingizwa chaka, niliichunguza Pari March, ni kampuni ambayo ni ya burudani, mchezaji anacheza kwa huku akiburudika kutokana na kiwango kidogo cha kuanzia Sh300.