Bahati Bukuku aeleza chanzo cha ukimya wake

Muktasari:

Bahati Bukuku ametamba na nyimbo kama ‘Dunia Haina Huruma’, ‘Majaribu’, ‘Maamuzi’, ‘Umewazidi Wote’ na nyingine nyingi, amesema alikuwa kimya kwa muda mrefu hajatoa wimbo wowote kutokana na majukumu mengine kumbana, lakini ameshatunga nyimbo kadhaa, amezirekodi na anasubiri kuziachia tu.

MWANAMUZIKI mkongwe wa nyimbo za Injili, Bahati Bukuku amesema hakuna tofauti kati ya nyimbo za Injili za sasa hivi na zile za zamani.

Bukuku ameliambia Mwanaspoti kuwa anakutana na swali hilo kwa watu wengi hivyo kudhani asilimia kubwa ya watu wanaamini muziki wa Injili umebadilika, kitu ambacho sio kweli.

“Nadhani hakuna tofauti yoyote ya nyimbo za Injili za zamani na sasa, kwa sababu muziki ni uleule. Mabadiliko yaliyopo ni ya kawaida kwa sababu lazima muziki ukue na hata tulivyokuwa tunaimba sisi, tuliowakuta walikuwa wanaimba tofauti, ila na sisi tukauboresha kwa hiyo hata hawa wanatakiwa watafute staili yao wenyewe ili muziki uzidi kuwa mzuri zaidi,” alisema.

Bahati Bukuku ametamba na nyimbo kama ‘Dunia Haina Huruma’, ‘Majaribu’, ‘Maamuzi’, ‘Umewazidi Wote’ na nyingine nyingi, amesema alikuwa kimya kwa muda mrefu hajatoa wimbo wowote kutokana na majukumu mengine kumbana, lakini ameshatunga nyimbo kadhaa, amezirekodi na anasubiri kuziachia tu.

“Ni kweli nilikuwa kimya sana, ila kwa sasa hivi nimeshaandaa nyimbo na nimesharekodi, nasubiri muda ufike ili niweze kuziachia, ukimya wangu ulitokana na kuwa bize na majukumu mengine,” alisema.