Liverpool yapata pigo la mwaka

Muktasari:

Sadio Mane atakuwa nje ya uwanja kwa wiki sita, baada ya kuumia misuli, hivyo atakosa mechi 10 zikiwemo za Ligi Kuu England na Ligi ya Mabingwa Ulaya.

London, England. Sadio Mane atakuwa nje ya uwanja kwa wiki sita, baada ya kuumia misuli, hivyo atakosa mechi 10 zikiwemo za Ligi Kuu England na Ligi ya Mabingwa Ulaya.
Klabu ya Liverpool imepata pigo katika harakati ya kuwania ubingwa wa Ligi Kuu England msimu huu mbele ya vigogo vingine Manchester City, Manchester United, Tottenham Hotspurs na Chelsea.
Liverpool itamkosa mchezaji huyo wa kimataifa wa Senegal hadi Desemba, mwaka huu baada ya kupata maumivu ya misuli.
Mane, 25, Adam Lallana na Nathaniel Clyne ambao ni majaruhi, wataigharimu Liverpool ambayo tangu kuanza msimu huu imeshindwa kutamba.
Kocha Mherumani Jurgen Klopp, atamkosa mshambuliaji huyo katika mechi mbili za Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Maribor na Sevilla na mechi sita za Ligi Kuu England.
Liverpool imekuwa katika mazingira magumu tangu kuanza msimu huu, baada ya kushinda mechi moja kati ya saba katika Ligi Kuu England.
Mane amefunga mabao matatu msimu huu. Klopp atakosa mechi mbili muhimu dhidi ya Tottenham Hotspurs na Chelsea.
Mchezaji huyo alitoka dakika ya 87 kutokana na maumivu aliyopata katika mchezo wa kuwania kufuzu Fainali za Kombe la Dunia Jumamosi iliyopita dhidi ya Cape Verde