Nyota wa Prisons atoboa siri Mudi kwenda Yanga

Muktasari:

Dirisha dogo la usajili litafunguliwa rasmi kesho, hivyo ni wakati wa timu za Ligi Kuu Tanzania Bara na zile za madaraja ya chini kuanza kuboresha vikosi vyao.

Dar es Salaam.Pacha wa Mohammed Rashid katika kikosi cha Tanzania Prisons, Eliuter Mpepo amekili kuwepo na uvumi wa mshambuliaji mwezake kutakiwa na Yanga.
Dirisha dogo la usajili litafunguliwa rasmi kesho, hivyo ni wakati wa timu za Ligi Kuu Tanzania Bara na zile za madaraja ya chini kuanza kuboresha vikosi vyao.
Yanga inahusishwa kumtaka mshambuliaji huyo wa Prisons aliyefunga mabao matano (5) katika Ligi Kuu bara hadi sasa.
"Hizo taarifa siyo ngeni, tumekuwa tukizisikia lakini bado haijawa rasmi, Rashid ni rafiki yangu sana na nilivyozisikia nilimfuata na kumuuliza kwa lengo la kujua kama ni kweli Yanga imefanya naye mawasiliano.
"Naye alistuka na kuonekana hakuna anachojua, siwezi kumsemea ila ngoja tuone nini kitatokea kwa sababu ndiyo kwanza kipindi cha usajili kinaelekea kuanza," alisema Mpepo.
Mpepo amefunga mabao mawili katika ligi, amekuwa akicheza na Rashid kwenye eneo la ushambuliaji la Tanzania Prisons na kufunga wote kwa pamoja jumla ya mabao saba katika michezo tisa ya Ligi Kuu Bara hadi sasa.