Wachezaji wanusurika kifo wakishangilia ubingwa


FURAHA nusura igeuke huzuni baada ya basi la wazi walilokuwa wakilitumia wachezaji na maofisa wa mabingwa wapya wa Ligi Kuu ya Serbia, Red Star Belgrade, kuwaka moto wakati likipita mitaani.
Wachezaji wa Red Star Belgrade walikuwa na mzuka mwingi wakati wakishangilia ubingwa wao wa 28, lakini ghafla basi hilo la wazi likashika moto kwa kile kilichoelewa hitilafu ya umeme.
Hata hivyo, wachezaji na mabosi walilazimika kila mmoja kuruka kutoka ndani ya gari hilo katika harakati za kuokoa maisha.
Mabingwa hao wapya walimaliza kazi ya kupigania ubingwa na kukabidhiwa taji hilo katika uwanjani Rajko Mitic kwa ushindi wa mabao 5-1 dhidi ya Vozdovac mjini Kalemegdan.
Hata hivyo, taarifa zingine zinaeleza kuwa hitilafu hiyo itakuwa imesababishwa na staili ya ushangiliaji wa mashabiki wake kwa kurusha fataki hewani.
Serbia ndiko anakotokea kiungo wa nguvu wa Manchester United, Nemanja Matic, ambaye pia ndio nahodha wa timu ya Taifa ya nchi hiyo.