Simba washusha kiungo Mzambia

Muktasari:

Mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu Bara msimu huu wanahaha kutafuta kiungo mpya wa ushambuliaji tena wa kigeni.

Dar es Salaam. Habari ndio hiyo, kama ulikuwa Simba unadhani wanatania katika kusuka kikosi kipya na imara msimu huu sahau hilo.
Mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu Bara msimu huu wanahaha kutafuta kiungo mpya wa ushambuliaji tena wa kigeni.
Katika kusaka kiungo bingwa hao wameaguki kwa Mzambia Chama Clatous ambaye kama mambo yatakwenda sawa atasaini mkataba wa kuitumikia klabu hiyo.
Chama anacheza katika klabu ya Lusaka Dynamos ya Zambia amependekezwa na kigogo mmoja wa kamati ya usajili baada ya kuzungumza na kocha Masoud.
Chama mwenye miaka 27 na kabla ya kucheza Al Ittihad alikuwa katika klabu ya Zesco United 2014-17 ambapo alicheza mechi 34 na kufunga mabao 16.
Chama anauwezo wa kufunga, kupiga pasi ndefu na fupi anaweza kutumia nguvu na kushindana na viungo wagumu huenda kwani amekuwa akifanya hivyo katika Ligi ya kwao huenda akasaini mkataba wa miaka miwili.
Wachezaji wote wa Simba jana walifanyiwa vipimo katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili na Chama alikuwa miongoni mwa wachezaji hao.
Kikosi cha Simba kitaondoka usiku wa leo Jumamosi kuelekea Uturuki ambapo wataweka kambi mpaka Agasti 20 Chama atajumuishwa katika msafara wa nyota hao.
"Ndio ameingia alfajiri na amekuja kwa ajili ya Simba na tumemfuatilia siku nyingi na leo tunamfanyia vipimo na wachezaji wengine wote kama atakuwa sawa kwa kila kitu tutamsainisha mkataba," alisema kiongozi huyo wa Simba.
"Mimi bado sijamuona maana sijaenda huko kwenye vipimo, lakini nikiwa naye nitafahamu mambo mengi, lakini kwa sasa sina lolote la kusema dhidi yake," alisema Meneja wa Simba Richard Robert 'Mwana'.