Simba msitafute sababu Kirumba

Muktasari:

Simba inacheza kesho Alhamisi na Mbao FC, lakini meneja wa Uwanja wa CCM Kirumba, Jonathan Mkumba anahakikisha sehemu ya kuchezea inakuwa vizuri ili ikitokea wamefungwa wasitafute sababu.

Mwanza. Uongozi wa Uwanja wa CCM Kirumba upo kwenye hatua za mwisho kukamilisha sehemu ya kuchezea kwa ajili ya mechi ya Ligi Kuu Bara kati ya Mbao FC na Simba SC ambapo leo Jumatano Uwanja unafyekwa.

Meneja wa uwanja huo,  Jonathan Mkumba amesema kuwa wanaandaa uwanja ili uwe katika hali nzuri kuepusha malalamiko hasa kwa timu ya Simba kama itapoteza mechi hiyo itakayochezwa kesho Alhamisi.

Mkumba amesema, mara nyingi timu kama Simba na Yanga zinapocheza kwenye uwanja huo zikipoteza malalamiko yao uwanja kuwa mbovu.

"Hatutaki malalamiko kama watafungwa, maana imekuwa ni kawaida timu kubwa kulalamika viwanja vibovu pale tu wanapopoteza mechi zao za mikoani,"alisema Mkumba.

"Hivyo nimeweka vijana  wafyeke nyasi uwanjani na kuuweka uwanja kwenye mandhari nzuri ili hata jioni ya leo Jumatano watakapokuja kufanya mazoezi ya mwisho wakute upo vizuri  kuondoa malalamiko yao."

Mwanaspoti imeshuhudia meneja huyo akitoa maelekezo kwa vijana watakaofyeka ikiwa ni pamoja na umwagiliaji wa maji uwanjani hapo.