Duh! Kichuya anapika hadi harusini babake

WINGA wa Simba, Shiza Kichuya, kumbe mjanja bwana, kwani licha ya kupambana na mabeki uwanjani ili kuibeba timu yake, lakini nje ya hapo jamaa ni bonge la mpishi.

Kichuya amelifahamisja Mwanaspoti kwamba kabla ya watu kumfahamu kisoka, alikuwa anapika kwenye harusi na shughuli nyingine kama za sendoff, misiba na hata kipaimara, alikoitwa kutoa huduma yake.

Alisema hata sasa shughuli hizo zinaendelea kama kawaida, japo amewakabidhi watu wa kumsaidia ili akili zake zikae vema uwanjani.

“Nafanya vitu hivyo kwa makubaliano maalumu na mtu anavyotaka shughuli yake kama iwe ya kifahari ama kawaida. Ikitokea nikaboranga basi namrejeshea gharama zake, sipendi kufanya kazi zangu mtu anakuwa ananiwekea kinyongo,” alisema.

“Haya ni maisha huwezi kukaa ukalemaa, nadhani umri wangu unaniruhusu kujenga uchumi, utakaonisaidia mbeleni nikizeeka, ndio maana sibagui kazi ya kufanya ilimradi tu iwe halali na huo upishi nina watu wanaonisaidia.

“Hizo dili nilizipiga sana mjini Morogoro, siwezi kuweka wazi napata kiasi gani, lakini mtu yeyote akihitaji nimfanyie kazi nipo tayari, ataifurahia tu iwe Dar es Salaam au Morogoro.”

Akiizungumzia Ligi Kuu Bara,  Kichuya mwenye mabao matano hadi sasa msimu huu, alisema ligi itakapoendelea wataifuata Ndanda FC ya Mtwara kiakili.

“Mechi itakuwa ngumu kwani nao wamesajili, kikubwa ni nidhamu ya kazi ili tuweze kushinda na kuendelea kuongoza ligi,” alisema.