Luiz atishia kuondoka Chelsea kisa namba

Muktasari:

Beki huyo Mbrazili amemwambia kocha huyo kwamba anataka nafasi yake kwenye kikosi cha kwanza kama itashindikana basi hatakuwa na kitu cha kuendelea kukifanya hapo Stamford Bridge, ataondoka!

LONDON, ENGLAND. KAMA mbwaimbwai, unaambiwa. David Luiz ameamua kumaliza utata baada ya kumfuata kocha wake huko Chelsea, Antonio Conte kumaliza bifu na kuweka hadharani matakwa yake.

Beki huyo Mbrazili amemwambia kocha huyo kwamba anataka nafasi yake kwenye kikosi cha kwanza kama itashindikana basi hatakuwa na kitu cha kuendelea kukifanya hapo Stamford Bridge, ataondoka!

Luiz na Conte wamekuwa kwenye bifu kubwa siku za karibuni ambapo Mbrazili huyo alipigwa chini kwenye kikosi cha kwanza baada ya kumkosoa kocha wake juu ya mbinu zake katika mechi ya kipigo kutoka kwa AS Roma katika Ligi ya Mabingwa Ulaya Oktoba mwaka huu. Luiz alionyesha kutofurahishwa pia wakati alipofanyiwa sub katika mechi ya nyumbani dhidi ya Wataliano hao.

Tangu sakata hilo kuibuka, Luiz sasa amekuwa gumzo akiwindwa na klabu kibao ikiwamo Real Madrid na Bayern Munich, huku kocha Jose Mourinho akimtaka pia beki huyo wa kati aende akaongeze nguvu huko Old Trafford.

Mtu wa karibu na Luiz alisema: "David ni kama mchezaji mwingine yeyote yule anataka kucheza. Hivyo kwa sasa anasubiri tu kuona nini kitatokea."