Bato la AliKiba, Yondani usipime kabisa

Muktasari:

  • Katika mchezo wa Timu Kiba dhidi ya Timu Samatta, AliKiba aliwaongoza wenzake huku upande wa  Timu Samatta, Mbwana Samatta ndio alikuwa akiwaongoza wenzake.

Dar es Salaam. Unaambiwa kama ulikuwa unajua AliKiba ni mwanamuziki tu basi utaumbuka, jamaa bado yupo vizuri katika katika soka usipime.
Katika mchezo wa Timu Kiba dhidi ya Timu Samatta, AliKiba aliwaongoza wenzake huku upande wa  Timu Samatta, Mbwana Samatta ndio alikuwa akiwaongoza wenzake.
Kiba ndio alikuwa akiongoza mashambulizi kwa upande wa timu yake, alionekana kuwa fiti vilivyo na kumsumbua beki kisiki wa Yanga, Kelvin Yondani.
Yondani alikuwa akipata tabu ya kumkaba Kiba kutokana na kasi yake aliyonayo pamoja na umbo kubwa ambalo lilikuwa likimpa tabu katika kumzuia.
Katika kipindi chote cha kwanza ilikuwa bato la hali ya juu huku mashabiki wakivutiwa kuona msanii huyo akipambana na beki huyo kisiki nchini.
Katika kipindi cha pili timu Samatta ilifanya mabadiliko kwa kumtoa Kelvin Yondani, lakini hata hivyo Kiba hakuonyesha cheche kama aliyoanza nayo.
Timu ya Kiba ilipata penalti, lakini umakini wa Kiba katika upigaji ulikuwa mdogo na kufanya penalti hiyo kupaa licha ya kwamba alifanikiwa kumuuza kipa Juma Kaseja.