Azam kupiga ndondo Iringa, Mbeya

Dar es Salaam. AZAM FC imeanza kujiandaa na Ligi Kuu ya Vodacom, ilianza kufanya ziara yao nchini Rwanda na kucheza mechi mbalimbali za kirafiki ikiwemo dhidi ya wenyewe wao Rayon Sport na sasa wanaelekea Nyanda za Juu Kusini.

Mechi ya kwanza kwenye kanda hizo itachezwa Julai 22 dhidi ya Mbeya City ikiwa ni mwaliko maalumu kutoka klabu hiyo inayomilikiwa na Halmashauri ya Jiji la Mbeya ambayo Julai 19 watazindua rasmi jezi zao zitakazotumika msimu ujao.

Meneja wa Azam FC, Philip Alando aliliambia Mwanaspoti kuwa baada ya kumaliza mechi hiyo watacheza na timu zilizopanda daraja ambapo Julai 24 watacheza na Njombe Mji na kumaliza mechi ya mwisho Julai 26 dhidi ya Lipuli ya Iringa.

"Baada ya hapo timu itarejea jijini Dar es Salaam ambapo wachezaji watapata mapumziko ya siku mbili na kuingia kambini kuendelea na mazoezi kabla ya kucheza tena na Ruvu Shooting na Mtibwa Sugar, mechi ambazo zitachezwa Chamazi," alisema Alando