Ali Kiba amtia ndimu Banda

Muktasari:

  • Banda ametoa ahadi hiyo ikiwa ni siku moja baada Ali Kiba kufunga ndoa ya aina yake na mrembo Amina Khalef kule Mombasa, Kenya.

BEKI wa Baroka FC ya Afrika Kusini, Abdi Banda jana Ijumaa ilikuwa siku yake ya kuzaliwa, lakini amekuja na bonge la ‘surprise’ baada ya kutamka bayana siku atakayofunga ndoa na mchumba wake, Zabibu Kiba ambaye ni mdogo wa Ali Kiba.

Banda ametoa ahadi hiyo ikiwa ni siku moja baada Ali Kiba kufunga ndoa ya aina yake na mrembo Amina Khalef kule Mombasa, Kenya.

Beki huyo wa zamani wa Simba alisema, amepata mzuka na shamrashamra za harusi ya Kiba, jambo ambalo linamfanya kutamani kukamilisha kuanza maisha mapya na Zabibu, ambaye wamekuwa pamoja kwa muda mrefu. Sasa Banda ametamka bayana kwamba, ifikapo Agosti mwaka huu, atakuwa amekamilisha kila kitu na Zabibu atakuwa mkewe wa ndoa.

“Haya mambo ya harusi ni mipango na kwa upande wangu kama Mungu atajaalia nimepanga kufunga ndoa mwezi wa Nane (Agosti) hapo kila kitu kitakwenda sawa, Ali ameanza na mimi nitamaliza,” alisema Banda ambaye pia ni beki wa Taifa Stars. Akizungumzia harusi hiyo ya Ali Kiba, Banda amesema: “Nimependa hiyo hitu kwani ni jambo jema kuhalalisha aisee.”