Kocha Njombe Mji aikumbuka Mbao FC
Dar es Salaam. Kocha wa Njombe Mji, Ally Bushiri amesema haikuwa kazi nyepesi kuwaondoa Mbao FC ambao walifika fainali wa msimu uliopita kwenye Kombe hilo la Shirikisho la Azam (ASFC).
Njombe Mji ilifanikiwa kuiondosha Mbao katika raundi ya 16 bora kwa mikwaju ya penalti 6-5 baada ya kutoka sare ya bao 1-1 kwenye dakika tisini za mchezo, uliochezwa kwenye uwanja wa Sabasaba.
Katika mchezo huo, Njombe ndiyo waliokuwa wa kwanza kujipatia bao kipindi cha kwanza kupitia kwa Ditram Nchimbi, Mbao ilisawazisha bao hilo kipindi cha pili kupitia kwa Said Said.
“Mbao ni moja ya timu ngumu, japo nipo kwenye kipindi cha kukijenga kikosi change lakini nilitumia mbinu mbadala ya kucheza kimahesabu makali, mbinu za mchezo wa mtoano huwa ni tofauti na mbinu za kawaida.
“Ukipoteza inamaana unatolewa kwa hiyo tulikuwa na umakini mkubwa kwenye uchezaji wetu japo kuna makosa madogo madogo ambayo tuliyafanya,” alisema Bushiri.