Hamasa Stars kama zote tu

Muktasari:

Mshindi wa mechi mbili za nyumbani na ugenini baina ya Taifa Stars na Sudan atafuzu moja kwa moja kwenye Fainali za Chan.

SHIRIKISHO  la Soka Tanzania (TFF), limetangaza kukamilika kwa maandalizi ya mchezo baina ya Taifa Stars na Sudan huku likiwaomba Watanzania kujitokeza kwa wingi uwanjani kuishangilia timu ya taifa
Akizungumza katika mkutano wa waandishi wa habari leo, Katibu Mkuu wa TFF, Wilfred Kidao alisema shirikisho limejipanga vyema kuhakikisha Stars inapata ushindi kwenye mechi hiyo.
"TFF kwa maana ya kiutendaji tumejipanga vizuri kwa ajili ya mechi hiyo. Timu tumeiweka kwenye kambi yenye hadhi ya juu katika Hoteli ya nyota tano ya Hyatt Hotel na wachezaji wote wako kwenye hali nzuri.
Masuala mengine yote kwa maana ya posho na yale ambayo tunahitajika kufanya tumeshayatimiza hivyo kilichobaki ni mchezo wenyewe.
Kikubwa tunawaomba Watanzania kujitokeza kwa wingi kwa ajili ya kuipa hamasa na sapoti timu. Na ni jambo jema kama watawahi mapema kabla ya kuanza kwa zoezi la kupasha misuli, muda ambao kisaikolojia mchezaji utayari wa mechi kwa mchezaji unaanza," alisema Kidao