Azam FC kufunga Azam Complex

Muktasari:

Uwanja wa Azam Complex hivi karibuni umekuwa ukitumika na timu mbalimbali kucheza mechi zake.

MABOSI wa klabu ya Azam FC wameshtukia jambo kwenye uwanja wao wa Azam Complex na fasta wakaamua kufanya kitu ambacho kitazidi kuufanya uwanja huo kunoga zaidi.
Mabosi hao wamebaini nyasi bandia zilizopo kwenye uwanja hio zimechakaa na sasawameanza mikakati ya kufumua upya kapeti lao la nyasi hizo ili kuurejesha kwenye kiwango bora.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Azam, Abdulkarim Amin 'Popat' alisema wataufunga uwanja wao kwa muda wa miezi miwili ili kurekebisha nyasi zao.
"Ligi ikisimama kupisha michuano ya Kombe la Chalenji basi sisi ndio tutafanya marekebisho, kuna Mapinduzi Cup, hivyo tunaamini kabisa kwamba tutatengeneza kwa kutumia muda huu," alisema.
Popat, aliongeza kwa kusema majani ya uwanja huo tayari yalishamaliza muda wake wa kutumika na ndio maana wametumia muda huu kufanya marekebisho.
"Wataalam wetu wataanza kufika Desemba  Mosi na Pili, kisha mara moja wataanza kazi hii ya kuweka nyasi mpya katika uwanja wetu huu," alisema.