Singano hana kinyongo na Azam FC

Muktasari:

Pamoja na Azam FC kumwachia aende Ramadhan Singano, mchezaji huyo ameonekana kuwa na kibari baada ya kuwepo taarifa ya kutakiwa na Simba na Yanga.

LICHA ya Azam FC kumpa mkono wa kwaheri Ramadhan Singano, ameonyesha kutokuwa na kinyongo baada ya kutamka kuwa timu hiyo imeweka alama ya kukumbukwa katika maisha yake ya soka.
Singano alijiunga Azam FC baada ya kuachana na Simba mwaka 2015 anasema kila timu ambayo amewahi kuichezea katika maisha yake ina mchango mkubwa kwa wakati sahihi aliokuwepo.
Kuhusu kuachwa Azam FC, anasema kwake sio kitu kinachomuumiza akisisitiza kwamba kwa mchezaji yoyote yule duniani, anapokuwa kwenye timu anakuwa anatambua kwamba ipo siku ataondoka.
"Kuondoka kwangu Azam FC ni jambo la kawaida na la kimpira, hivyo ni sehemu ya kazi, naamini watakaochukua nafasi zetu watakuwa na mchango mkubwa wa kuhakikisha klabu hiyo inafanya vyema kwenye michuano ya kimataifa na ligi kuu Bara.
"Azam FC nitaikumbuka kwa mengi kama mchango wao mpaka nilipofika leo, kumaliza kwangu mkataba na kutoongezewa nachukulia kwa upande wa kwenda kujipanga upya na kuona nitaanza vipi maisha mengine mapya nje ya timu hiyo"anasema.
Wakati Azam FC wakimuacha, kuna habari kwamba winga huyo anahitajika na timu zingine za Ligi Kuu.