Nyota Serengeti Boys wamlilia Dk Mengi

Muktasari:

Dk Mengi mbali na kuwa mmiliki wa makampuni ya IPP Media, alikuwa mlezi wa kikosi cha timu ya taifa ya vijana chini ya miaka 17 'Serengeti Boys'amefariki usiku wa kuamkia leo
Alhamisi katika nchi za Falme za Kiarabu.

Dar es Salaam. Wachezaji wa timu ya taifa ya vijana ya Tanzania chini ya miaka 17, 'Serengeti Boys' wanamlilia aliyekuwa mlezi wao, Dk Reginald Mengi aliyefariki dunia
usiku wa kuamkia leo Alhamisi.
Mengi alikuwa kama baba wa kikosi hicho cha Serengeti Boys na ni miongoni mwa wadau waliokuwa wamewaahidi zawadi nyingi vijana hao kama pesa na magari katika fainali zaAFCON, lakini walizikosa baada ya kushindwa kufuzu nusu fainali ambayo ingewapa nafasiya kushiriki Kombe la Dunia.
Wakizungumza katika nyakati tofauti wachezaji hao wakiongozwa na mshambuliaji, Kelvin John 'Mbappe' amesema kitu kikubwa anachomkumbuka Mengi ni maneno yake anayozungumza kwa Lugha ya Kiingereza ya I can, I must, I will.
"Mengi namkumbuka kwa mambo mengi kwanza maneno yake hayo ya ushindi ambayo yanakufanya mtu ujitambue, ujipange kitu cha kufanya katika maisha yako ili ufanikiwe,"alisema Kelvin ambaye kwa sasa amechaguliwa kwenye kikosi cha Taifa Stars chini ya Kocha Mkuu Emmanuel Amunike.
Beki wa kushoto wa Serengeti Boys, Mohammed Omary alipoambiwa taarifa ya kifo cha Mengi alishtuka.
"Heh! Kumbe amefariki. Namkumbuka kwa mengi ya Mzee Mengi hasa kutokana na maneno yake ya kufariji watu na kuwafutia wengi hasa kisa cha maisha yake ambayo yalikuwa duni, lakini hakukata tamaa, alipambana mpaka mwisho na ndiyo sababu akafika alipo sasa,"alisema Omary.
 "Nakumbuka alisema, wapo watu walimkatisha tamaa lakini hakujali na hakutaka mtu amuharibie ndoto zake na katika mambo yote hayo alimtangulisha Mungu mbele.
"Alitusisitiza kuachana na mambo ya ushirikina kwa sababu hata hao watu wanamtaja Mungu pia kutoiacha elimu kwa sababu pamoja na kipaji lolote linaweza kutokea ukashindwa kufikia malengo."
Naye kipa wa Serengeti Boys, Shaaban Kimwaga amesema, anamkumbuka Mengi kwa mambo mengi.
"Nakumbuka nilimjua kwa mara ya kwanza tulipokuwa tunakwenda Burundi. Alijitamburisha kuwa yeye ni mlezi wetu alituunga mkono na kutusaidia kwa mambo mengi. Alituahidi na kutupa vingi,"alisema Kimwaga.