Sio Kagere, Morrison mpango mzima Mhilu

Muktasari:

Licha ya Kagere na Morrison kuwa habari ya mjini kwa mashabiki wao, beki wa Kagere Sugar, David Luhende imekuwa tofauti kwake yeye ametazama wazawa zaidi.

BEKI wa Kagera Sugar, David Luhende amesema licha ya Meddie Kagere wa Simba na Bernard Morrison wa Yanga, kuonekana kupendwa na mashabiki lakini haoni kama wana maajabu ya kutisha kuliko wazawa.

Amesema habezi kiwango chao isipokuwa anaamini kuna wachezaji wazawa wenye uwezo zaidi yao lakini wanachukuliwa poa wakati walipaswa kupewa sapoti kwa ajili ya faida ya timu ya Taifa 'Taifa Stars'.

"Wachezaji wa kigeni wamewasoma mashabiki wa Tanzania wanapenda nini, ndio maana unakuta wanatafuta vituko ili mladi tu wapate kiki yakusemwa mitaani, ukichunguza baada ya muda wanakuwa wa kawaida,"

"Morrison na Kagere kwani wana uwezo wa juu ninachosisitiza mimi kuna wachezaji wazawa wenye uwezo kama wao, waungwe mkono ili wapate morali yakujituma  zaidi," amesema.

Ameulizwa ni straika gani anayesumbua kwa msimu huu, amemtaja Yusufu Mhilu anayecheza naye timu moja kwamba kwa kasi yake ya mabao angekuwa Simba na Yanga angekuwa habari ya mjini.

"Mbona kuna wachezaji kibao wanaofanya vyema kwa nafasi ya ushambuliaji kama Paul Nonga ama kwa sababu yupo Lipuli, naamini wakikaza wazawa watachukua kiatu cha dhahabu msimu huu," amesema.