Mkude ampa mzuka nyota wa Lipuli

Muktasari:

Kiungo wa Lipuli, Ally Liungo ana mahesabu makali ya kuhakikisha kipaji chake kinafika mbali baada ya kumtazama Jonas Mkude kwa muda mrefu na kuvutiwa na uwezo wake.

PAMOJA na kwamba huu ni msimu wa kwanza kwa kiungo wa Lipuli FC ya Iringa, Ally Liungo kucheza Ligi Kuu Bara ni miongoni mwa wachezaji ambao wameonyesha uwezo wa hali ya juu na kuwa msaada ndani ya kikosi chake.

Liungo amesema kwamba kupata kwake nafasi kwenye kikosi cha kwanza cha Lipuli, kumetokana na juhudi za kutaka kuonyesha kipaji chake ili aweze kufika mbali.

Amesema wakati amekwenda kufanya majaribio kabla ya kusajiliwa alikuwa anawasoma wachezaji ambao wanacheza namba yake kisha akaenda kuongeza kasi ya mazoezi ambayo yamemsaidia.

"Baada ya kusajiliwa nilianza kama masihara nikakuta kocha ananielewa ikanipa morali ya kuendelea kupambana kuona nafikia ndoto zangu,"amesema.

"Nimejiunga na Lipuli nikitokea timu ya Supa Mahakama ya Kirombelo, najua hapa ni daraja tu ila ipo siku ambayo nitaishi ndoto zangu,"amesema.

Amemtaja Jonas Mkude kwamba ndiye alikuwa anavutiwa na kipaji chake na kwamba anaamini atacheza zaidi yake
"Lengo langu nikucheza nje ya nchi, naamini nitavuka hadi  uwezo wa mchezaji niliyekuwa natamani kuwa kama yeye,"amesema.